Na Mwandishi Wetu
Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ikiongozwa na Naibu Gavana wa Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, imefanya kikao na wadau mbalimbali kujadiliana kuhusu mpango wa kuanzishwa kwa kampuni ya utoaji na usimamizi wa dhamana za mikopo itakayojulikana kama Tanzania Credit Guarantee PLC.
Kikao hicho kilichofanyika leo, tarehe 12 Machi 2026, katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam, kimewakutanisha wadau kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Kampuni za Bima, Mifuko ya Pamoja ya Uwekezaji wa Mitaji, Mifuko ya Pensheni pamoja na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).

Mpango wa kuanzishwa kwa kampuni hiyo unalenga kuendana na ukubwa na kasi ya utekelezaji unaohitajika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuimarisha uchumi wa Tanzania na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa.
Vilevile, kampuni hiyo itasaidia kutenganisha majukumu ya Benki Kuu ya udhibiti na utoaji wa dhamana za mikopo, hivyo kuondoa mgongano wa maslahi na kuboresha ufanisi wa kiutendaji. Pia itahamasisha ubunifu pamoja na kuongeza uwezo wa taasisi husika kujibu kwa haraka mahitaji ya soko.
Kwa sasa, Benki Kuu ya Tanzania inasimamia mifuko miwili ya udhamini wa mikopo ambayo ni Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Mauzo ya Nje (Export Credit Guarantee Scheme – ECGS) na Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SME Credit Guarantee Scheme – SME-CGS).
Serikali ilianzisha mifuko hiyo kwa lengo la kudhamini benki na taasisi za fedha ili kuimarisha utoaji wa mikopo kwa wakopaji wenye miradi yenye tija lakini wanaokabiliwa na upungufu wa dhamana. Lengo kuu ni kuwezesha mazingira rafiki ya kukuza na kuendeleza miradi ya maendeleo, kuongeza ajira, kuimarisha upatikanaji wa fedha za kigeni kupitia mauzo ya nje na kuchangia ukuaji wa pato la Taifa.






