-TANESCO yaeleza matumizi ya umeme katika magari, bajaji na pikipiki
-Pikipiki ya umeme hutumia uniti 3 pekee kusafiri hadi kilometa 130
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Wananchi wamehimizwa kutumia umeme katika vyombo vya usafiri ili kupunguza gharama za uendeshaji na kuchangia matumizi ya nishati safi na yenye ufanisi.
Akizungumza Julai 5, 2026 katika Banda la TANESCO kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Saba Saba), Afisa Uhusiano wa TANESCO, Bi. Amanda Tagame, amesema teknolojia ya usafiri wa kutumia umeme haipo kwenye magari pekee, bali pia inapatikana katika bajaji na pikipiki.
Ameeleza kuwa pikipiki ya umeme hutumia wastani wa uniti tatu za umeme zenye thamani ya takribani shilingi 1,500 na inaweza kusafiri hadi kilometa 130 kwa chaji moja, jambo linaloifanya kuwa chaguo la gharama nafuu na lenye ufanisi kwa watumiaji.
‘’ Tunaposema endesha kwa umeme hatumaanishi katika magari pekee, bali pia katika bajaji na piki piki, ukitumia nishati ya umeme kwenye pikipiki ni nafuu sana ,hutumia wastani wa uniti 3 za umeme zenye thamani ya takribani shilingi 1,500, zinazowezesha kusafiri hadi kilometa 130”alifafanua Bi. Tagame.
Bi. Tagame amesema TANESCO itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya umeme katika sekta ya usafiri ili kuwawezesha kufanya maamuzi yanayowanufaisha kiuchumi na kuunga mkono matumizi ya nishati safi.





