Na Israel Mwaisaka, JamhuriMedia, Rukwa
JESHI la Polisi mkoani Rukwa linamshikilia Maiko Sosolo Kazikulima (35), mkazi wa Kijiji Cha Mashete kata ya Mashete wilayani Nkasi kwa kosa la kumuua mkewe Victoria Mputa (32) kwa kumpiga na rungu kichwani na kusambaratisha ubongo wake akimtuhumu mkewe kuwa na mahusiano ya kimapenzi na watu wengine.
Kwa mujibu wa Taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa Rukwa SACP, Shadrack Masija, ni kuwa tukio hilo limetokea Septemba 8, 2026 majira ya saa 3 usiku, wakati wakitoka kilabuni pamoja na ndipo ulipozuka ugomvi miongoni mwao uliohusishwa na wivu wa kimapenzi na kupelekea mwanamke huyo kuuawa.
Alifafanua kuwa mtuhumiwa ambaye alikua mume wa marehemu wakiwa njiani kabla hawajafika nyumbani mzozo mkubwa kati yao uliibuka huku mume akiendelea kumtuhumu mkewe kwa kuwa na mahusiano na wanaume wengine kiasi cha kuchukua maamuzi hayo yaliyopelekea kifo kinyume cha sheria.
Kamanda Masija amedai kuwa mtuhumiwa anaendelea kuhojiwa na Polisi na kuwa upelelezi ukikamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo zinazomkabili.
Sambamba na hilo amewataka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi katika kuwabaini wahalifu na kuwa katika kipindi hiki wamekua wakipata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa wananchi kitu kilichopelekea wahalifu wengi kunaswa na kufikishwa mbele ya chombo vya sheria.


