Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam

KATIKA juhudi za kuwainua wajasiriamali nchini, Benki ya CRDB kupitia programu yake ya IMBEJU, kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, imeendelea kutoa elimu ya fedha kwa wajasiriamali ili kuwajengea uwezo wa kusimamia kwa ufanisi biashara na mikopo wanayoipata.

Wito wa kuchukulia elimu ya fedha kama silaha ya mafanikio umetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya IMBEJU, Fadhili Bushagama, wakati wa hafla ya kufunga semina maalum ya mafunzo ya awali kwa wajasiriamali wanaotarajiwa kunufaika na mkopo wa asilimia 10 kutoka Halmashauri.

Bushagama amesema kuwa fedha ni muhimu, lakini elimu ya kifedha ni msingi wa kuzijua na kuzitumia vyema fursa zinazowazunguka wajasiriamali.

“Tunatambua kuwa mkopo bila elimu ni mzigo. Ndiyo maana tunahakikisha kila anayeguswa na Imbeju anapitia mafunzo haya,” alisema.

Wajasiriamali waliopata nafasi ya kushiriki, kama Jackline Mkina na Ally Mvunyo, waliushukuru mpango wa Imbeju na kueleza namna elimu waliyoipata imewasaidia kubadili mtazamo wao wa kibiashara.

“Kwa kweli Imbeju imetufungua macho. Leo tunaweza kupanga matumizi, kuweka akiba na kurudisha mikopo kwa wakati,” alisema Jackline kwa furaha.

Kwa upande wake, Mvunyo aliongeza kuwa maarifa aliyoyapata yameweza kumsaidia kutambua maeneo yenye changamoto katika biashara yake, na hivyo kuzuia hasara kubwa.

Semina hiyo ililenga kuwafundisha wajasiriamali mbinu za uwekezaji wa akiba, uendelezaji wa miradi, pamoja na namna ya kushughulikia changamoto za vikundi vyao.

Elimu hiyo imeelezwa kuwa endelevu, huku wale waliopokea wito kutoka halmashauri wakitarajiwa kuitwa tena hivi karibuni kwa awamu nyingine ya mafunzo ya kina.

Kupitia IMBEJU, CRDB inalenga kuwafikia zaidi vijana na wanawake, ikiwa ni mkakati wa kuchochea ustawi wa jamii na kuimarisha uchumi wa taifa. Programu hii imejikita si tu katika kutoa mitaji, bali pia kuhakikisha elimu inatangulia ili kila mjasiriamali awe na msingi imara wa mafanikio.