Yah: Saba Saba na vinyozi na wapigadebe tunakwenda wapi?
Wanangu, nawashukuruni kwa kusoma mambo ya zamani pamoja na kwamba yanawakera, kwa sababu wengi wenu mnaona kama historia na ambayo labda mengine hayakuwahi kuwaingia vichwani kwamba yaliwezekana na yalitekelezeka.
Niliwahi kuwaandikia barua hii kuwakumbusha juu ya barua ambazo tulikuwa tukiandika, na ilichukua mwezi au zaidi kumfikia aliyeandikiwa. Barua hiyo ilikuwa na ujumbe mzito haiyumkiniki zilikuwa habari za uzazi, ndoa, vifo, majanga na hata tukio la furaha kijijini kwetu.
Baada ya miaka kadhaa ya Uhuru tulianzisha Shirika la Posta na Simu ambalo wakati huo simu zote zilikuwa zikiunganishwa Dodoma kwenda katika mikoa mingine. Hii ilikuwa njia ya haraka sana ya mawasiliano, lakini haikuwa kwa watu wote, bali wachache tu waliochukulia jambo lao ni la haraka sana.