Na Peter Haule na Saidina Msangi, WF, Dodoma

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ameipongeza Kampuni ya Puma Energy Tanzania kwa jitihada zake za kuongeza uwekezaji na kuboresha uendeshaji wa kampuni, hatua iliyowezesha Serikali kupata gawio la Sh. bilioni 15.

Mhe. Balozi Omar alitoa pongezi hizo jijini Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Puma Energy Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Bi. Fatma Abdallah, katika Ofisi za Wizara ya Fedha Treasury Square.

“Utoaji wa gawio ni ishara kwamba kampuni inaendelea kufanya vizuri na kupata faida, jambo ambalo pia linaongeza mchango wake katika maendeleo ya nchi,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa Serikali imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha sekta ya nishati inaendelea kuwa imara na kufanya vizuri, licha ya changamoto zinazojitokeza katika soko la nishati duniani.

Alisema hatua hizo zinalenga kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma za nishati kwa gharama nafuu na kupunguza athari za mabadiliko ya bei za nishati.

Aidha, alisema Serikali itaendelea kuhakikisha kunakuwa na ushindani wa haki katika sekta ya nishati ili kulinda maslahi ya wananchi, wakati huo huo kuhakikisha mapato ya Serikali hayaathiriki na ushindani usio na tija.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Bi. Fatma Abdallah, aliipongeza Serikali kwa jitihada inazochukua katika kuhakikisha sekta ya nishati inaendelea kuwa imara na wananchi wanapata huduma stahiki.

Alisema Puma Energy Tanzania itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Serikali na kuimarisha shughuli zake ili kuongeza mchango wake kwa Taifa, ikiwemo kuongeza gawio kwa Serikali.

Bi. Abdallah pia alisema jitihada zinazofanywa na Serikali zimechangia kushuka kwa gharama za mafuta, jambo ambalo linaendelea kuwa na manufaa kwa wananchi na uchumi kwa ujumla.