Takribani watoto 800 hugundulika kuwa na saratani kila mwaka

Waziri wa Afya Ummy Mwalimu leo Septemba 23,2022 ameweka wazi kuwa, kila mwaka takriban watoto 800 hugundulika kuwa na ugonjwa wa Saratani nchini Tanzania hivyo kuchangia ongezeko la vifo vinavyotokana na ugonjwa huo.

Waziri Ummy amesema hayo katika kikao na Taasisi ya Global HOPE iliyoko Texas nchini Marekani katika mkutano wa pembezoni baada ya Mkutano Mkuu wa 77 wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) unaoendelea New York, nchini Marekani.

“Kila mwaka takriban watoto 800 hugundulika kuwa na ugonjwa wa Saratani nchini Tanzania, lakini kama Serikali tumeendelea kuboresha matibabu ya Saratani kwa watoto ili kuokoa maisha yao.” amesema Waziri. Ummy.

Ameendelea kusema kuwa, inakadiriwa kuwa watoto wenye saratani wanaoendelea kuishi zaidi ya miaka miwili kuanzia kugundulika ni kati ya asilimia 20 hadi 40, huku katika nchi zilizoendelea ni zaidi ya asilimia 80, hii ni kutokana na kuchelewa kufanya uchunguzi, kuasi matibabu, gharama za usafiri na malazi, uchache wa vituo vinavyofanya uchunguzi na uhaba wa watumishi wenye ujuzi.

Aidha, Waziri Ummy amemshukuru Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Global Hope Dkt. David Poplack Kwa msaada wanaoipatia Serikali ya Tanzania ambapo wanaoendelea kufadhili programu na kuwajengea uwezo watumishi hususan katika fani za ubingwa bobezi wa matibabu ya Saratani na magonjwa ya damu zaidi ya 10, na kutoa vifaa vya uchunguzi katika hospitali ya Muhimbili.

Sambamba na hilo, Waziri Ummy ameiomba Taasisi hiyo kuongeza idadi ya watanzania wanaopatiwa ufadhili wa mafunzo ya utoaji huduma za Saratani Kwa kada za Uuguzi, Madaktari ,Wafamasia na Wataalamu wa maabara.

Kwa upande mwingine, Waziri Ummy amemwomba kujengea uwezo hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya katika kutoa huduma hizo Kwa kujenga na kuipatia vifaa vya kisasa vya huduma za Saratani.

Kwa upanda wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Global Hope Dkt.Polack alieleza kuwa, Taasisi hiyo ipo tayari kushirikiana na Serikali ya Tanzania kutekeleza miradi mbalimbali ya kuimarisha huduma za Saratani nchini.