Na Heri Shaaban, JamhuriMedia, Dar es Salaam

MANISPAA ya Temeke imeshika nafasi ya kwanza kwa kukusanya mapato mengi zaidi ya shilingi bilioni 53 kabla Juni 31, mwaka huu wa fedha 2025/2026.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani Manispaa ya Temeke, Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Jamary Satura, alisema hayo katika Baraza la Madiwani ukumbi wa Idd Nyundo Temeke.

“Tumefanikiwa kukusanya mapato mengi zaidi ya shilingi bilioni 53 tumefanikiwa na kuvuka lengo ninawashukuru Madiwani wa Temeke na watumishi wangu kwa ushirikiano mzuri “alisema Satura.

Mkurugenzi Jamary Mrisho Satura, alisema kutokana na kuvuka lengo la ukusanyaji mapato wanaweza kutekeleza bajeti yote ya mwaka huu wa fedha katika miradi ya maendeleo ikiwemo sekta ya afya na sekta ya elimu na miundombinu ya barabara.

Satura aliwataka madiwani Manispaa ya Temeke ambao bado kutekeleza bajeti waseme ili waweze kutekeleza Ilani katika miradi yao.

Mkurugenzi Satura alitumia fursa hiyo kuwapongeza Madiwani na watumishi wake wa Manispaa ya Temeke kwa ushirikiano wao katika ukusanyaji mapato ya Serikali.

Alisema wananchi wa Manispaa ya Temeke wana kiu ya maendeleo wameweza kulipa tozo na kodi mbalimbali ambapo alisema katika mapato ya ndani wanajenga shule tano za Gholofa na hospitali zenye adhi ya wilaya chamazi na yombo ,Tuangoma.

Kwa upande wake Meya wa Manispaa ya Temeke Abdalah Mtinika, alipongeza uongozi wa Manispaa hiyo pamoja na Mkurugenzi Jamary Satura kwa utendaji bora wa kazi kufikia malengo.

Meya Abdalah Mtinika alisema yeye na madiwani wake wapo tayari kufanya kazi usiku na mchana katika kuisaidia Serikali iweze kufikia malengo yake katika kumsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.