Na Mwamvua Mwinyi,JamhuriMedia,Kibaha

WANAWAKE mkoani Pwani wameaswa kuvunja ukimya na kuungana kupinga vitendo vya ukatili kwa watoto na kuwaasa kuwakemea watoto wao kujiepusha kwenda vibanda umiza ambavyo vingine huwa vikionyesha video zisizo na maadili.

Akizungumza katika hafla ya Generation Queen’s (Mwanamke Sahihi) kukabidhi baiskeli 15 zenye thamani ya milioni sita kwa watoto wenye ulemavu Kibaha ,Rachel Chuwa kutoka sekretariet ya mkoa wa Pwani ameeleza mwanamke nyumbani ndio Mwalimu wa watoto hivyo wajitahidi kuwafuatilia na kukemea watoto wanapojiingiza kwenye mambo maovu.

Amewataka jamii na wanawake wote kijumla ,kushiriki kupinga vitendo vya ukatili kwa kuvunja ukimya na mzunguko mzima wa ukatili kwa kutumia vyombo vya sheria bila kuficha matukio yanayotokana na ukatili hali inayosababisha kuongeza idadi ya matukio hayo kwenye jamii.

Rachel aliwapongeza Mwanamke Sahihi kwa kumkomboa mtoto mwenye ulemavu na Kuwa sehemu ya kumkomboa mwanamke.

Akitoa taarifa ya kikundi Cha Generation Queens ,Mwenyekiti wa Generation Queen’s ,Betty Msimbe ameeleza, wametoa baiskeli hizo 15 lakini lengo ni kutoa baiskeli 100 zenye thamani ya milioni 70 .

Alisema ,wamekusudia kumkomboa mtoto mwenye ulemavu kutokana na wengi wao kukosa mahitaji muhimu na wengine kuficha hali inayosababisha kukosa haki mbalimbali ikiwemo elimu.

“Tumepata maombi mengi kutoka kwa watoto hao ,sisi pekee hatuwezi !!,tuwaombe taasisi binafsi , jamii pamoja na wadau waguswe kusaidia kushirikiana na sisi kusaidia vifaa vya watoto wenye ulemavu”amesisitiza Msimbe.

Msimbe aliwaasa wazazi na walezi wanaoishi na watoto wenye ulemavu wasiwafiche watoto wao kwani wanawakosesha haki wanazostahili kupata Kama walivyo watoto wasio na ulemavu.

Mwenyekiti huyo, alimuomba Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuangalia namna ya kuwapatia shule au maeneo ambayo watawekwa watoto wenye ulemavu ili waweze kuwafuatilia maana wapo ambao majumbani hawapati mahitaji sahihi.

Vilevile Msimbe, ameelezea kuhusu maendeleo ya kikundi hicho tangu kianzishwe mwaka 2019 ,na kusema kwasasa kina hisa milioni 23.5 na wameweza kukopeshana milioni 74.9 .

Mjumbe wa kikundi Cha Mwanamke Sahihi ,Nancy Godwin alitoa Rai kwa wanawake kujitokeza kujiunga na vikundi vya akinamama kwani vinasaidia kujikomboa kiuchumi na kupata mikopo kirahisi.

By Jamhuri