CHADEMA YAZIDI KUTEKETEA, MADIWANI WAKE WAWILI WAJIUNGA CCM

Madiwani wawili kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakiwa na makada 20 wa Vyama vya Upinzani wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera wamekabidhi kadi zao kwa Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kyerwa na kuamua kuhamia ndani ya chama hicho.

Madiwani hao waliohama ni Sadath Jeremiah aliyekuwa Diwani wa kata Kibale na Tulakila Twijuke aliyekuwa Diwani wa kata Bugomora na Katibu Mwenezi wa CHADEMA wilaya ya Kyerwa, ambapo wamesema wameridhishwa na utendaji wa Rais Magufuli na watendaji wake hivyo wameamua wenyewe bila kuhongwa na mtu yeyote kuunga mkono jitihada  za utendaji zinazoonyeshwa na CCM.

Kwa upande wake Katibu wa Siasa na Uenezi wa CCM mkoa wa Kagera Amimu Omary amesema wamezindua rasmi zoezi la kupokea Madiwani ambapo wameshapeleka maombi ya kupokelewa ndani ya chama hicho  japo mengine bado wanayajadili na kuongeza kuwa leo wamepokea jumla ya wanachama 22, wawili ni Madiwani wa CHADEMA, wawili ni Wenyeviti wa Vitongoji kupitia TLP na kumi na nane ni wanachama wa Chama cha CHADEMA.