HATUPANGI KUSHINDWA, TUNASHINDWA KUPANGA (13)

Unapanga na Mungu anapanga

“Mja hutaka, Mola hujalia.” Ni msemo wa Waingereza. Katika mipango yetu ni vizuri kumuingiza Mungu. “Ukitaka Mungu acheke, mwambie juu ya mipango yako,” anasema Woody Allen. 

Ukipanga mipango usisahau kusema: “Mungu akipenda.” Bila maneno hayo unamchekesha Mungu. Ukipanga mipango midogo sana unamchekesha Mungu. Mungu wetu anatuwazia makubwa.

Kwa kawaida binadamu hupanga na Mungu anapanga. Unapanga kukwepa mateso fulani lakini Mungu anakupitisha kwenye tanuri la mateso ili kukuimarisha. “Mungu anaweza kuwaweka watu kwenye maji marefu, lengo si kuwaangamiza, bali kuwasafisha,” anasema Plautus.

Mwanamuziki, Michael Jackson, alipanga kuishi zaidi ya miaka mia. Aliweka mikakati ya kiafya ya kuweza kutimiza lengo hilo. Bahati mbaya aliaga dunia akiwa na umri wa miaka 50. Ni katika mtazamo huu maneno ya Kitabu cha Mithali yanatupa mtazamo mpana wa maisha: “Binadamu hupanga mipango yake, lakini kauli ya mwisho ni yake Mwenyezi Mungu.” (Mithali 16: 1). Kwa vile Mungu ana kauli ya mwisho, tumuombe atusaidie katika kila tufanyalo. Bila Mungu hatuwezi lolote.

Majina tunayomuita Mungu yatufundishe mengi kumhusu yeye. Anaitwa Muumba. Tukumbuke kuwa Muumba ndiye Muumbua. Muumba ndiye awezaye kuumbua au kutufisha. Mwanadamu hawezi kujidai kuwa yeye ndiye Muumba. Mungu anaitwa pia Jalali au Jalia, kwani yeye ndiye anayetujalia.

Katika msingi huu tuna methali kama: “Mungu kasema niombe nikupe.” ; “Mungu hamkoseshi mja wake yote.” Utumie akili yako kupanga ya kesho lakini usitegemee akili yako tu. “Umtegemee Bwana kwa moyo wako wote, usitegemee akili yako wewe; katika njia zako zote, umkumbuke yeye, naye atasawazisha mapito yako.” (Mithali 3: 5-6). 

Katika mtazamo huo Benjamin Franklin anasema: “Kadiri ninavyozidi kuishi, ninaona ushahidi zaidi unaonishawishi wa ukweli huu: Mungu anatawala mambo ya watu.” Ukishinda kwenye mambo ya Mungu, Mungu anashinda kwenye mambo yako. Tunapomkaribisha Mungu katika maisha yetu tunapenda atusaidie kwa vile tuna wajibu mkubwa wa kutia nguvu zetu, maarifa yetu na utaalamu wetu. Kuna hadithi ya watoto wawili ambao walichelewa shuleni. 

Wakiwa njiani mmoja alitoa pendekezo: “Tusimame tusali, tumuombe Mungu atusaidie kufika shuleni katika muda unaohitajika.” Mwingine alisema: “Tukimbie kwa nguvu zetu zote na tusali kumuomba Mungu atusaidie wakati tunakimbia.” 

Mungu huwasaidia wanaoweka juhudi kujikwamua na kupiga hatua. “Farasi hutayarishwa kwa vita, lakini ushindi wamtegemea Mwenyezi Mungu.”

Kumbuka Mungu anatengeneza njia ambapo hakuna njia. Usikose kumuingiza katika mipango yako. Ukipata mateso usikose kumuingiza Mungu katika mipango yako. Upendo wa Mungu kwetu wakati mwingine hautukingi na mateso, bali unatupitisha kwenye mateso. Unapopanga kumbuka kuna wakati wa Mungu na wakati wa binadamu. “Mungu hachelewi sana na hawai sana, lakini anakuja kwa wakati.” (R.T. Kendall). Kumbuka unapanga na Mungu anapanga.

Mungu ametupa akili; tuitumie vizuri na tuumize kichwa kupanga na kutafuta suluhisho. Kuna hadithi ya mwanafunzi aliyewasili akiwa amepanda ngamia wake hadi kwenye hema la bosi wake. Aliteremka kutoka kwenye ngamia wake hadi ndani ya hema akainama na kumwambia bosi wake: “Tumaini langu kwa Mungu ni kubwa kiasi kwamba nimemwacha ngamia wangu nje bila kumfunga, nikiwa na uhakika kuwa Mungu hulinda masilahi ya wale wanaompenda.” 

Bosi alitoa amri: “Nenda ukamfunge ngamia wako! Mungu hawezi kusumbuliwa kwa kufanya mambo ambayo unaweza kabisa kuyafanya wewe mwenyewe.” Mungu akusaidie, anahitaji mchango wako kwanza. Fanya vizuri sana unavyoweza. Linalobaki mwachie Mungu.