IGP amekwisha kuhukumu,iundwe tume huru

Askari Polisi watatu, mlinzi wa kampuni binafsi na mtu aliyetajwa
kwa jina la Hamza, wamefariki dunia katika tukio la kurushiana
risasi jijini Dar es Salaam wiki iliyopita.
Kutokana na mauaji hayo yaliyotekelezwa na Hamza, Rais Samia
Suluhu Hassan, ameliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi
wa tukio hilo.
Muda mfupi baadaye, Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali
(IGP) Simon Sirro, akasema uchunguzi unafanywa kubaini
sababu za raia huyo kufanya uhalifu huo.
Wakati wa kuaga miili, IGP Sirro, akionekana mwenye hasira, alitoa
kauli kali zenye mwelekeo wa kuwalaumu watu waliomzaa
Hamza, na ‘akashauri’ wazazi wengine wasizae ‘kina Hamza’.
Watu waliomtazama na kumsikiliza walitambua uchungu alionao
wa kupoteza askari. Kupoteza askari watatu ni pengo kubwa.
Mungu awarehemu.
Matamshi yake kuhusu Hamza na tukio zima la mauaji, yanaibua
maswali. Kauli za IGP zimekuja ilhali mitaani kila mmoja
akiwa na mtazamo wake kuhusu mauaji hayo. Mengi
yanazungumzwa. Wapo wanaosema kitendo cha Hamza
kuwalenga polisi na kuwaacha mamia ya watu wengine
kinaashiria jambo.
Kwa kuwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama,
Rais Samia, ameagiza uchunguzi ufanywe, tunaamini kuwa
kazi hii haipaswi kuachiwa Jeshi la Polisi wao wenyewe,
hasa ikizingatiwa kuwa tayari kauli za IGP Sirro ni kama
zimekwisha kumhukumu Hamza.
Kwa kuheshimu utawala wa sheria na haki, tunashauri kazi hii ya
uchunguzi ifanywe na chombo huru – tukirejea mfano wa Tume
ya Kijaji iliyoundwa na Rais wa wakati huo kuchunguza mauaji
ya wafanyabiashara wa madini kutoka mkoani Morogoro.
Kuundwa kwa tume hiyo kunaweza kusaidia kupata majibu ya
maswali mengi yanayoulizwa na wananchi kuhusu vyanzo
halisi vya tukio hili na mengine yanayowahusisha baadhi ya
polisi katika nchi yetu.
Kwa namna IGP alivyoonyesha, si rahisi uchunguzi
utakaowashirikisha zaidi polisi ukapokewa kwa mikono miwili
na wananchi ambao kwa miaka yote wamependa nchi yao iwe
ya amani na utulivu.
Lakini pia tunawaomba viongozi wetu wawe na maneno ya faraja
kwa ndugu wa wahalifu, kwa sababu si kweli kuwa ukiwa na
ndugu mhalifu, lawama lazima ziwaangukie ndugu zake.
Hamza alikuwa Mtanzania, na rekodi zinaonyesha alikuwa mtu
muungwana na hata jeshi linaloongozwa na IGP Sirro
likaridhia kummilikisha bastola. Hamza alikuwa kada mahiri
wa CCM, aliyehakikisha anakitumikia chama hicho kwa hali
na mali na kwa nyakati zote.
Kitu gani kimembadili ghafla na kuwa muuaji, ndicho hicho
wananchi wangependa kukijua. Ili kukijua, kunahitajika
uchunguzi huru ambao kwa mtazamo wetu hauwezi kuwapo
kama kazi hiyo watapewa Jeshi la Polisi chini ya IGP Sirro,
ambaye amekwisha kuonyesha upande wake. Tunaamini tume
huru ndiyo inaweza kuleta majibu sahihi ya kadhia