JWTZ watanda Mirerani

*Sasa hakuna kutorosha jiwe nje ya uzio
*Wazalendo furaha, wakwepa kodi kilio

SIMANJIRO

NA MWANDISHI WETU

Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
(JWTZ) limepokewa kwa shangwe kwenye
dhima yake mpya ya kulinda migodi ya
tanzanite, Mirerani mkoani Manyara.
Uwepo wa askari wa JWTZ wenye silaha na
magari ya deraya katika eneo hilo, ni
utekelezaji wa maagizo ya Amiri Jeshi
Mkuu, Rais John Magufuli, Aprili 6, mwaka
huu alipokuwa akizindua ukuta uliojengwa
kuzunguka eneo hilo. Ukuta huo wenye
kimo cha mita tatu na urefu wa kilometa

24.5; umegharimu Sh bilioni 6.
Katibu wa Chama cha Wachimba Madini
Mkoa wa Manyara (MAREMA), Tawi la
Mirerani, Abubakari Madiwa, amezungumza
na JAMHURI mwishoni mwa wiki na
kusema wamefurahi mno kuona eneo hilo
linalindwa na JWTZ.
“Kuna magari ya deraya na askari wenye
silaha za kawaida, kwa kweli wachimbaji
wamefurahi ingawa yapo malalamiko
madogo hasa kwenye upekuzi kwa kina
mama.
“Wamefurahi kwa sababu wanasema ni
tofauti na polisi. Si wasumbufu sana,
wanataka ukweli tu. Ukifika unaambiwa
nenda pale, lipia, ondoka, hakuna
longolongo,

” amesema Madiwa.

Ameulizwa kwanini polisi wanalalamikiwa
na wachimbaji wadogo na kujibu:
“Wanasema [wachimbaji] wao huwa
wanataka hela, mara hela ya kula, mara
hela ya maji, lakini Jeshi (JWTZ) hawana
hayo.”
Hata hivyo, Madiwa amesema kumekuwapo
malalamiko ya hapa na pale hasa kutoka
kwa kina mama.

“Wanaona kupekuliwa hadi kwenye ‘duka’
[sehemu za siri] si jambo zuri.
Wanapendekeza ingekuwa vizuri
wakatumia scanner ambazo zina uwezo wa
ku-detect chuma au madini,

” amesema.

Ukiacha dosari hiyo aliyosema
inarekebishika, katibu huyo amesisitiza:
“Jeshi tumelipokea kwa mikono miwili.
Tuliahidi na tunaendelea kuahidi kuwa
tutafanya kazi nalo kwa karibu. Sisi
tutakuwa walinzi namba mbili ili kuhakikisha
kuwa hakuna madini yanayotoroshwa. Awali
tulitaka tulinde sisi lakini tukawa tunatupiana
mpira hasa kwenye gharama za kuwalipa
walinzi, lakini Mheshimiwa Rais (Magufuli)
aliposema JWTZ watalinda, kwa kweli
tulifurahi na sasa tunaiona kazi yao,

amesema.
Wiki iliyopita, Msemaji wa JWTZ, Kanali
Ramadhan Dogoli, alisema idadi ya askari
imeongezwa kwenye migodi ya Mirerani ili
kuimarisha ulinzi. Akakanusha kuwapo kwa
vifaru.
“Hatuwezi kuimarisha ulinzi hata mara moja
kwa kutumia vifaru, vifaru na ukuta
haviendani kabisa, vifaru viko mbali

[Arusha],

” amesema.

Baadhi ya wachimbaji wadogo
waliozungumza na JAMHURI
wamepongeza uamuzi wa kupelekwa askari
wa JWTZ kulinda eneo hilo.
“Sasa mambo yako sawa, ukifika getini
unaonyesha kitambulisho unaingia.
Kulitolewa amri wachimbaji mwisho saa 5
usiku watoke migodini, lakini JWTZ
wamekuja wamesema kuchimba ni saa 24
alimradi kusiwe na uvunjifu wa taratibu.
“Ulinzi ni mkali kweli kweli, hakuna mtu
anapita na jiwe [tanzanite]. Tumeona kuna
watu, hasa kina mama wanakutwa na mawe
wameweka sehemu za siri. JWTZ
wamejipanga kweli kweli. Habari kwamba
ukuta umevunjwa ili kutorosha madini si za
kweli. Utaanzaje kutorosha madini kwa hali
hii? Tunaomba waendelee kuimarisha
ulinzi,

” amesema mchimbaji mmoja.
Anatetea uwepo wa magari ya deraya,
akisema baadhi ya wachimbaji wadogo ni
wahalifu sugu wanaotumia hata bunduki,
kwa hiyo ulinzi unapaswa kuwa imara kama
ilivyo sasa.
Katika hatua nyingine, Wizara ya Madini

imefanya mabadiliko madogo kwenye safu
ya uongozi wa Idara ya Madini Kanda ya
Kaskazini.
Mabadiliko hayo yamegusa nafasi ya
Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya
Kaskazini iliyokuwa ikishikwa na Adam
Juma.
Kwa muda mrefu Mirerani imekuwa haitulii
kutokana na migogoro mbalimbali
iliyowahusisha wachimbaji wadogo dhidi ya
wakubwa, na wachimbaji wote kwa jumla
dhidi ya serikali.
Wakati migogoro hiyo ikiendelea, serikali
imekuwa ikipoteza mabilioni ya shilingi
kutokana na kukithiri kwa biashara ya
magendo ya madini hayo ambayo hadi sasa
taarifa za kijiolojia zinaonyesha kuwa
yanapatikana Tanzania pekee.
Tume kadhaa zimekwisha kuundwa ili
kuleta suluhu ya kudumu, lakini
mapendekezo yake mengi yamekuwa
hayatekelezwi. Hata suala la ujenzi wa
ukuta lilikuwa kwenye mapendekezo ya
moja ya tume hizo – Tume ya Jenerali
Robert Mboma.
Tume hiyo iliundwa na aliyekuwa Waziri wa

Nishati na Madini, Edgar Maokola-Majogo,
baada ya kuwapo migogoro mingi ya
wachimbaji wakubwa na wadogo, utoroshaji
wa madini na kudorora kwa usalama katika
eneo hilo.
Mapendekezo mengine ya tume hiyo ni
kuhakikisha tanzanite inachimbwa na
wachimbaji wadogo Watanzania; na ikatoa
mfano:
“Tuige mifano ya nchi za Thailand kwa
madini ya Pink Ruby na Sri Lanka kwa
madini ya Sapphire, ambazo zimewaachia
wachimbaji wadogo kuchimba madini hayo
bila kuruhusu wawekezaji wakubwa
kuyachimba.”
Iliishauri serikali iwaondoe watu
wasiotakiwa eneo la mgodi, wasiokuwa raia,
wazururaji, wahalifu, wasiokuwa wachimbaji
na ambao si waajiriwa kwenye migodi.
Mapendekezo mengine ni kila mmiliki wa
mgodi au wa leseni ya eneo husika kutunza
takwimu za majina ya wafanyakazi wake,
zinazoonyesha jina la mfanyakazi na anuani
yake, tarehe na mwaka alioajiriwa.
Ikapendekezwa kila mfanyakazi kwenye
mgodi awe na kitambulisho na kuwapo

utaratibu wa kudhibiti uingiaji na utokaji wa
watu katika eneo la machimbo ya Mirerani.
Ikapendekezwa yafanywe marekebisho ya
Sheria ya Madini Na. 5 ya 1998 na Sheria
ya Mamlaka ya Kodi ili kuwepo wakaguzi
wa uchimbaji madini (mining inspectors) na
maofisa wa kudumu wa Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) kwenye migodi
watakaokuwa wanathibitisha kiasi cha
madini kinachozalishwa na mchimbaji na
kufuatilia mkondo wa madini kuanzia
machimboni hadi yanaposafirishwa.
Mapendekezo mengine ni kuanzishwa kwa
Ukanda wa Uzalishaji wa Bidhaa za Nje
(EPZ) Arusha au Mirerani ili kusaidia
kuongeza thamani ya tanzanite kwa kuwa
ukataji utakuwa unafanyika nchini na
kuongeza thamani na mapato ya serikali.