Mabingwa watetezi wa Kombe la Mapinduzi Azam FC imeanza vyema harakati za kutetea ubingwa wa michuano hiyo baada ya jana usiku kushinda mabao 2-0, timu ya Mwenge FC katika mchezo wa kundi A, uliopigwa uwanja wa Amaan Zanzibar.
Kocha wa Azam FC Aristica Cioaba, ameiambia Gaol, wamekwenda Zanzibar wakiwa na nia kutetea ubingwa wao ambao wameutwaa msimu uliopita kwenye uwanja huo huo wa Amaani.
“Tumekuja tukiwa na lengo moja la kutetea ubingwa wetu najua ni michuano ni migumu na timu nyingi zitakuwa zimetupania lakini najivunia kikosi bora tulichokuwa nacho msimu huu ambacho kina nipa matumaini ya kutetea taji hilo,” amesema Cioaba.
Kocha huyo raia wa Romania amesema ushindi dhidi ya Mwenge umezidi kuwaimarisha na kuwafanya wazidi kucheza kwa nguvu ili kupata matokeo ambayo yatawapeleka kwenye hatua zinazofuata za michuano hiyo.
Kwa ushindi wa jana Azam kwasasa ndiyo vinara wa kundi hilo la A wakiwa na pointi tatu sawa na Mwenge lakini wenye wana idadi nzuri ya mabao ya kufunga na kufungwa na Jumatano watashuka tena dimbani kuwakabili JKU ya Pemba kwenye uwanja huo huo wa Amaan.

By Jamhuri