Moja ya habari zilizochapishwa kwenye gazeti hili katika toleo lililopita ilihusu tamko la Mfalme wa Kwa Zulu Natal, Goodwill Zwelethini, aliyechanganya mambo.
  Mfalme Zwelethini anatajwa kuwa nyuma ya vurugu zilizotikisa Afrika Kusini wiki kadhaa zilizopita, ambako aliwaambia wananchi, “Wageni (xenophobia) ni lazima waondoke Afrika Kusini.”


  Japo kuna wakati alibadili kauli yake baada ya bila shaka alipokutana na kikwazo kutoka kwa viongozi wenzake wa kijadi, akiwamo kaimu kiongozi wa Jimbo la Gauteng, jijini Johannesburg, Qedani Mahlangu, baada ya hali kuwa mbaya.


  Kiongozi huyo anasema; “Waafrika Kusini lazima wapinge ushenzi huo,” jambo lililopokewa kwa mikono miwili na raia wa Zimbabwe walioandamana nje ya ubalozi wa Afrika Kusini mjini Harare, wakitaka kusitishwa kwa mashambulizi yanayoendeshwa dhidi ya xenophobia.
Maelfu ya Wazimbabwe huishi na kufanya kazi nchini Afrika Kusini, ambako takriban watu watano wameuawa kwenye mashambulizi yanayowalenga wageni.


  Ingawa inaelezwa hali imetulia lakini xenophobia bado wanajifungia ndani kutokana na hofu ya kuuawa na wenyeji ambao huwabaini wageni kwa salamu.
  Inalezwa kuwa wenyeji wakijua kuwa ni mgeni wanaanza kufanya vurugu, wengine wanapita kwenye maduka, kupora, kujeruhi na kuua. Kutokana na vitendo hivyo vya kikatili vinavyofanywa na raia hao wa Afrika Kusini dhidi ya raia wa kigeni, inaonesha bila shaka wamesahau fadhila walizozipata kutoka kwa Waafrika wenzao.


  Tunasema dhambi ya ubaguzi iliyokuwa inatendwa na makaburu dhidi ya watu weusi nchini humo iliyokuwa  ikilaaniwa kila eneo, ni aibu kutendwa na Waafrika dhidi ya wenzao.
  Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, katika moja ya hotuba zake akielezea ubaya wa ubaguzi, anaufananisha “sawa na kula nyama ya mtu” na kwamba mtu mwenye tabia hiyo hawezi kuacha kitendo hicho.


  Leo hii ndiyo tunaona vitendo hivyo visivyokubalika kufanywa na Waafrika waliojaa ubinafsi kama hawa ndugu zetu, raia wa Afrika Kusini.
  Tunasema ubinafsi kama huu unapaswa kulaaniwa na kila binadamu mpenda haki na kuheshimu utu, kwani kila mwanadamu ana haki ya kuishi mahali popote duniani.


  Wanaofanya vitendo hivyo vya kihuni nchini humo, wamelitia aibu taifa hilo na Bara la Afrika kwa ujumla, ambalo kabla wao walibaguliwa na Wazungu kabla ya viongozi wa nchi nyingine za Afrika kuja juu.

By Jamhuri