Madee – Nidhamu siri ya mafanikio

Msanii maarufu wa wa muziki nchini, Hamad Ally, maarufu kama  ‘Madee’  (pichani) kutoka katika kundi la Tip Top Connection la Manzese, jijini Dar es Salaam,  amesema kuwa siri ya mafanikio yake katika muziki ni nidhamu.

Akiongea jijini Dar es Salaam hivi karibuni mwanamuziki huyo ambaye amekuwa akifanya muziki kwa muda mrefu alisema kuwa ili kufanikiwa kwa kila kitu nidhamu ni kitu cha msingi.

 

Alisema kuwa kutokana na uzoefu wake katika kufanya shughuli za muziki, wanamuziki wengi hapa nchini wamekuwa wakipotea katika ramani ya muziki kutokana na kutokuwa na nidhamu katika kazi zao.

 

“Kufanya kazi kunahitaji nidhamu ya hali ya juu, tofauti na watu wengine wanavyifikiria kuwa muziki ni kitu cha kawaida,” Alisema msanii huyo wakati akihojiwa na moja ya kituo cha redio hapa nchini.

 

Kauli ya msanii huyo inakuja wakati muafaka ambapo kuna baadhi ya wasanii wa muziki ambao waliwahi kuwika katika tasnia hiyo lakini kwa sasa hawavumi tena kutokana na kile kinachoonekana dhaihiri kuwa walishindwa kuwa  na nidhamu katika kufanya muziki wao.


Hali ilivyo kwa sasa inaonyesha kuwa kuna wasanii wa muziki ambao waliwahi kushika kiasi kikubwa cha pesa na hata kuwika katika nchi za jirani, lakini kutokana na kutokuwa na nidhamu ya kazi, kwa sasa wamebakia katika historia ya kwamba waliwahi kutamba katika muziki enzi hizo.

 

Mbali na kutoa nyimbo nyingi akiwa na kundi la Tip Top Connection, Madee amekuwa akitamba na kibao chake cha Sio Mimi (Nani Kamwaga Pombe yangu) kabla ya kutoa kibao kingine kinachokwenda kwa jina la ‘Tema Mate Tuwachape’ ambacho pia kinapendwa na wapenzi wa muziki.