Bilionea wa Urusi ambaye ni mmiliki wa klabu ya soka ya Chelsea ya England Roman Abramovich, amesafiri kwa ndege hadi Tel Aviv baada ya kupata haki ya uraia wa Israel.

Maafisa wa uhamiaji wamesema kuwa alihojiwa wiki iliyopita kwenye ubalozi wa Israel mjini Moscow. Alikabiliwa na tatizo la kupata upya viza nchini Uingereza katika kinachoonekana kuwa na uhusiano na mzozo wa kidiplomasia kati ya Uingereza na Urusi.

Mzozo huo ulichangiwa zaidi na kupewa sumu kwa jasusi wa zamani na binti wake Sergei na Yulia Skripal.

Msemaji wa Abramovich hakutaka kuzungumza lolote kuhusiana na uraia wake mpya aliopewa katika taifa hilo la Mashariki ya Kati.

Bw Abramovich, mwenye umri wa miaka 51, atakua ndiye mtu tajiri zaidi nchini Israel sasa.

Viza yake ya uwekezaji nchini Uingereza inaripotiwa kuisha muda wake wiki kadhaa zilizopita, lakini serikali ya Uingereza imekataa kutoa kauli yoyote kuhusiana na ‘suala lake binafsi’.

Kucheleweshwa kwa utoaji wa viza mpya ya Bw Abramovich kunakuja wakati kukiwa na uhasama wa kiplomasia baina ya serikali za London na Moscow Baada ya kupewa sumu kwa jasusi wa zamani wa Urusi Sergei Skripal kusini mwa Uingereza.

Bwn Abramovich hakuhudhuria fainali za Kombe la FA katika uwanja wa Wembley mapema mwezi huu wakati Chelsea ilipoichapa Manchester United 1-0.

Vyombo vya habari vya Israeli vinasema kuwa tayari amepewa kitambulisho cha uraia nchini Israeli chini ya sheria ya kurudi nyumbani, ambayo inawawezesha wayahudi popote pale walipo duniani kurudi na kuwa raia wa Israel.

Gazeti la The Times nchini Israeli limeandika kuwa Bw Abramovich aliwasili Israeli Jumatatu na kwamba amehamia nchini humo.

 

By Jamhuri