Mwanafunzi wa sekondari ya Kalangalala mkoani Geita, Jonathan Mkono anayedaiwa kupigwa na mwalimu wake na kulazwa hospitalini, ameruhusiwa leo mchana Septemba Mosi, 2018.

Mkono alikuwa amelazwa hospitali tangu Agosti 30 baada ya kuchapwa na kupoteza fahamu na mwalimu wa nidhamu, Lawson Lechipya kwa kosa la kukutwa bwenini wakati wa vipindi jambo lililosababisha maumivu makali mwilini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya Mkoa wa Geita, Dk Moses Simon amesema mwanafunzi huyo ameruhusiwa baada ya afya yake kuimarika.

Amesema alifikishwa hospitalini hapo akiw ana maumivu baada ya kuchapwa fimbo mgongoni na kwamba hakuna eneo ambalo amevunjika.

“Daktari aliyempokea anasema alifika hapa akiwa na maumivu na alikuwa ana alama za kuchapwa mgongoni, alihudumiwa anaendelea vyema na sasa ameruhusiwa kurejea shuleni,” amesema.

Mwanafunzi huyo hakuweza kueleza hali yake kwa sasa baada ya walimu kumchukua na kumzuia kuzungumza na waandishi wa habari.

By Jamhuri