Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Paramagamba Kabudi akizungumza na wadau wa utafiti wakati akifungua Warsha ya siku mbili kwa watafiti wa Tanzania na kutoka nje iliyoandaliwa na Tasisi ya Utafiti ya REPOA leo jijini Dar es Salaam.
 Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Balozi  Amina Salim Alli akizungumza wakati anaongoza mjadala juu ya Uchumi wa Viwanda kufikia 2025
 Mtoa mada Mkuu wa Warsha hiyo Katibu Mkuu wa Umoja wa nchi za kusini mwa Afrika katika mausuala ya forodha(SACU), Paulina Mbala Elago akitoa mada yake juu kwanini Ushindani na jinsi ya kuufikia katika maendeleo ya viwanda katika nchi hizo.
 Mkurugenzi Mkuuu wa Tasisi  ya utafiti nchini Repoa Dk Donald Mmari akizungumza kabla ya kumkaribisha msemaji mkuu katika warsha hiyo ya kwanini ushindani juu ya viwanda kufikia 2025

Mkurugenzi Mtendaji wa Infotech Investment Group LTD , Ali Mufuruki akiongoza majadiliano ya hali ya biashara kwa sasa katika Warsha ya siku mbili iliyoandaliwa na Repoa nchini.
 Baadhi ya Washiriki waliohudhuria Warsha ya siku mbili iliyoandaliwa na Tasisi ya Utafiti nchini Repoa wakifuatilia mijadala mbalimbali
  Baadhi ya Washiriki waliohudhuria Warsha ya siku mbili iliyoandaliwa na Tasisi ya Utafiti nchini Repoa wakifuatilia mijadala mbalimbali
Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Paramagamba Kabudi  watatu kushoto akiwa katika picha ya  pamoja na wafanyakazi wa Taasisi ya utafiti nchini Repoa pamoja na wadau wa utafiti
WAZIRI wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi amesisitiza  Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea na hatua  za kuhakikisha kunakuwepo mazingira wezeshaji yatayofanikisha ujenzi wa viwanda nchini.
Prof.Kabudi amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua warsha ya utafiti iliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti ya REPOA ambapo mada kuu ilikuwa kujadili kuelekea jamii inayoendeleza viwanda 2025 : kwanini ushindani ni muhimu.
Pia kwenye warsha hiyo wadau wamejadili masuala ya kisera katika safari ya Tanzania kuelekea kwenye uchumi mseto na shindani ,ukiongozwa na viwanda , pamoja na kufikia nchi yenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 kama inavyotarajiwa kwenye dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.
akizungumza  baada ya ufunguzi wa washa hiyo Profesa Kabudi ametaja hatua mbalimbali ambazo Serikali inachukua katika kufanikisha ujenzi wa viwanda nchini na kufafanua kinachoendelea ni kuangalia jinsi gani kufanya bidhaa za Tanzania kuwa na ushindani kwenye soko la Dunia.
“Kuna mambo mengi ya kufanya katika kufanikisha ujenzi wa viwanda nchini .Nikumbushe tu wakati tunapata uhuru tulikuwa na viwanda viwili , hivyo jukumu la wakati ule ikawa ni kuanza kujenga viwanda na vilijengwa na kutoa ajira kwa wananchi.
“Hata hivyo ilipofika mwaka 1977 baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki tukarudi nyuma kidogo na baadae tukaingia kwenye vita dhidi ya Uganda ambapo tulitumia dola za Marekani milioni 5 kwenye vita.Hivyo tukawa hatuna fedha za kuendeleza viwanda.
“Pamoja na magumu ambayo tumeyapitia bado leo hii tunavyo viwanda vingi ingawa jukumu la Serikali ni kujenga viwanda zaidi ili kuboresha maisha ya wananchi wake katika kuleta maendeleo,”amesema Profesa Kabudi.
Amefafanua kwenye warsha hiyo wamejadili kwa kina hatua ambazo zinatakiwa kuchukuliwa katika kufikia malengo la kujenga viwanda na kuboresha maisha ya wananchi na kutumia nafasi hiyo kueleza tayari Serikali  imeanza kuchukua hatua kadhaa na baadhi ni elimu bure kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari ambayo inatoa fursa ya kuandaa wasomi kwa maendeleo ya nchi.
Pia amesema jitiahada nyingine zinaendelea katika ujenzi wa miundombinu ya barabara reli na bandari na kwamba miundombinu hiyo ni muhimu katika kujenga msingi imara wa kukuza na kuimarisha uchimi wa Tanzania.
Prof.Kabudi amezungumzia namna ambavyo Serikali imejikita katika kuboresha sekta ya afya ili kuwa na wananchi wenye afya imara watakaoshiriki kikamilifu katika kuleta maendeleo ya Taifa letu.Pia amegusia hatua zinazochukuliwa katika kuongeza nishati ya upatikanaji wa umeme kwa kuanzisha miradi mikubwa ya umeme na jana Rais John Magufuli amezindua mradi wa umeme wa Kinyerezi II.
Hata hivyo amesisitiza umuhimu wa ujenzi wa viwanda na kueleza huko nyuma wakati kukiwa na viwanda vya kutosha wanawake na wasichana wengi walipata ajira na kuondoa wale ambao wanaonekana wanazurula mtaani.Hivyo viwanda vikijengwa vitatoa ajira ikiwamo kwa wanawake.
Kuhusu malalamiko ya kodi kubwa , Profesa Kabudi amesema tayari Rais Magufuli ameshatoa maelekezo ya kuhakikisha kodi inakuwa yenye unafuu na juzi juzi amekutana na wafanyabishara kwa lengo la kujadili namna ya kutatua changamoto zilizopo kwenye sekta ya biashara na uwekezaji nchini ,hivyo kwenye eneo hilo mambo yanakwenda vizuri.
Kwa upande wa Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Balozi Amina Salim Ali amesema warsha hiyo imekuja wakati muhimu kwani yapo mambo ya kiseria ambayo yanajadiliwa na kuangalia namna ya kuboresha mazingira ya kuinua uchumi wa wananchi na kwa Zanzibar kuna hatua mbalimbali ambazo wamezichukua katika kuboresha maisha ya wananchi.
Amesema kwenye eneo la ujenzi wa viwanda, bajeti ya fedha ya mwaka huu kwa Zanzibar imejikita pia katika kufufua viwanda vya zamani  na ujenzi wa viwanda vipya kulingana na bajeti ya fedha ambayo wameitenga.
Pia wameamua kuimarisha kilimo cha bahari na katika hilo kuna baadhi ya vijana wapo nje ya nchi kwa ajili ya kujifunza mambo ya uvuvi hasa kwa kuzingati Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imenunua meli ya uvuvi kwa ajili ya kuwawezesha wavuvi.
Amesema wameimarisha kilimo cha mbogamboga kwani wanatambua kuna nchi za Uarabuni ambazo zinanunua mbogamboga kutoka Zanzibar huku akielezea hatua kadhaa ambazo zinachukuliwa na Serikali katika kuinua uchumi wa wananchi.
Kuhusu sera ya viwanda, amesema Zanzibar wameweka mikakati ya kuhakikisha wanaondoa changamoto zilizopo katika sekta ya viwanda na kuelezea namna ambavyo wameondoa urasimu kwa wanaotaka kufanya bishara na kuwekeza huku akizungumzia hatua ambazo wamechukua katika kuimarisha sekta ya utalii visiwani huo kwa kuhakikisha watalii wakienda wanakaa muda mrefu.
Wakati huo huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Repoa Dk.Donald Mmari amesema pamoja na kushuhudia ukuaji mzuri wa uchumi wa Tanzania kwa miaka 15 iliyopita, tafiti zinaonesha viwango vya tija katika sekta nyingi bado ziko chini na ushindani wake kulinganisha na nchi nyingine duniani bado haujaridhisha.
“Hata hivyo Tanzania ina uwezo wa kujiweka katika nafasi kubwa zaidi katika uchumi wa dunia  kwa kujenga uwezo wa ushindani ukiinuliwa na uwepo wa faida za kipekee ikiwemo eneo la kijiografia , wingi wa rasilimali za asili na utulivu wa kisiasa na kijamii.
“Lengo la warsha hii ni kujadili na kupata maoni yatokanayo ma tafiti na uzoefu wa nchi nyingine ili yatuongoze katika kushiriki na kuchangia zaidi kwenye juhudi zinazoendelea za kujenga uchumi wa viwanda ikizingatiwa kuwa mpango wa tatu wa maendeleo wa miaka mitato(2021/22-2025/26) utajikita katika kuimarisha uwezo wa Tanzania kushindana na kuongeza ukuaji wa uchumi kupitia mauzo ya nje ya nchi,”amesema Dk.Mmari.

By Jamhuri