Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli leo Alhamisi Mei 17, 2018 amefungua kituo cha Uwekezaji cha Suma JKT kilichopo Mgulani.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama wakiwemo mawaziri, pamoja na maafisa mbalimbali wa majeshi ya ulinzi na usalama hapa nchini.

Katika hafla hiyo, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Jenerali Venance Mabeyo ameeleza kuwa JWTZ linazidai sekta binafsi kiasi cha shilingi bilioni 40, huku taasisi za serikali zikidaiwa shilingi bilioni 3.4, jambo ambalo limekuwa likiwakwamisha katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo.

Ili kuliwezesha jeshi hilo kuwekeza katika miradi mbalimbali ya maendeleo, JeneraliMabeyo amemuomba Rais Magufuli apokee orodha ya wote wanaodaiwa na jeshi hilo, ili aongeze msukumo katika ulipaji wake.

Kutokana na ombi la Jenerali Mabeyo, Rais Magufuli ametoa muda wa mwezi mmoja kwa wadaiwa wote, kuhakikisha kuwa wamerejesha madeni wanayodaiwa na kuagiza baada ya kuisha kwa kipindi hicho mamlaka zinazohusika na ukusanyaji wa madeni pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kuwachukulia hatua kali wadaiwa wote.

“Niwaombe wote hawa wanaodaiwa madeni kwa kuchukua matreka, mimi niwape mwezi mmoja. Ndani ya mwezi mmoja wawe wamelipa. Baada ya mwezi mmoja vyombo vyote vya ulinzi na usalama vianze kuwasaka wote,” amasema Rais Magufuli.

By Jamhuri