RC Wangabo ashauri gereza la Mollo kujikita kwenye uzalishaji wa mbegu za mahindi na kuuza.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akisalimiana na maafisa magereza wa gereza la Kilimo Molo alipofanya ziara katika gereza hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia) pamoja na Mkuu wa Gereza la Molo ACP John Mwamgunda wakikagua ujenzi wa Zahanati mpya ya kisasa itakayotumika kwaajili ya wananchi na magereza ambayo ipo eneo la magereza.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akijadiliana na Katibu tawala wa Mkoa wa Rukwa Bernard Makali juu ya ujenzi wa Zahanati mpya ya magereza walipotembelea gereza hilo kujionea shughuli za kilimo zinazofanywa na gereza hilo pamoja na miradi mingine inayofanywa na gereza hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia), Mkuu wa Gereza la Molo ACP John Mwamgunda (katikati) na Katibu tawala wa Mkoa wa Rukwa Bernard Makali wakizungukia miradi iliyopo ndani ya eneo la gereza la kilimo la Molo lililopo kata ya Molo Manispaa ya Sumbawanga.

 

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amelishauri gereza la kilimo la Mollo kuona umuhimu wa kujikita kwenye uzalishaji wa mbegu ili kuuza na gereza hilo kuweza kujiendesha na kupambana na changamoto mbalimbali zilizopo katika gereza hilo.

Amesema kuwa katika mikoa ya nyanda za juu kumekuwa na shida ya uuzwaji wa mbegu feki na kupelekea malalamikomengi toka kwa wananchi lakini kwa kutumia nguvu kazi iliyopo katika gereza hilo wanaweza kupata soko hilo kama watajikita kwenye uzalishaji huo.

“Tumekuwa tunahangaika mbegu hapa kwa mikoa ya Rukwa na Katavi, tunaweza tukajikita kwenye gereza hili na kuzalisha mbegu kwa wingi kwaajili ya matumizi ya mkoa mzima na majirani, hivyo ndio vitu vya kufikiria, tunaweza kuzalisha mazao lakini hata mbegu pia,” Alisema.

Mh. Wangabo Ameyasema hayo alipofanya ziara katika gereza hilo lililopo kata ya Mollo, Manispaa ya Sumbawanga ili kujionea shughuli za kilimo za gereza hilo ambalo kwa mwaka huu wa mavuno limepata magunia ya mahindi 4058 na hulisha magereza matatu ya mikoa ya Rukwa na Katavi.

Nae mkuu wa gereza hilo ACP John Mwamgunda amesema kuwa gereza linalima mazao ya mahindi ya mbegu nay a chakula kati ya ekari 350 hadi 400 na maharage hulimwa kati ya ekari 20 hadi 30 na bustani ya mboga kati ya ekari 2 hadi 3 na kuwa mpaka sasa wana ziada ya magunia ya mahindi ya chakula 3263 ambayo yanaweza kuhimili hadi msimu ujao wa mavuno.

“Pamoja na kuwa na maeneo hayo vitendea kazi bado ni vichache na baadhi vilivyopo vimechakaa, hivyo tunahitaji kuongezewa vitendea kazi,” Alimalizia.