Mataifa 32 yaliyofuzu kucheza Kombe la Dunia nchini Urusi, tayari yamegawanywa katika makundi
manane yenye timu nne kila moja, huku presha ikiendelea kupanda kila kukicha. Makundi hayo ni:
Kundi A
Kundi hili lina mwenyeji wa mashindano hayo, Urusi sambamba na Saudi Arabia, Misri na Uruguay.
Ndani ya kundi hili Urusi ndiyo nchi pekee iliyo chini kisoka katika viwango vya FIFA ikishika nafasi ya 65
ikifuatiwa na Saudi Arabia, ambayo iko katika nafasi ya 63, Misri na Uruguay wakiongoza kundi hili kwa
kuwa nafasi ya 21 katika ubora duniani.
Tathmini zinaonesha kuwa Urusi ana kazi ya ziada kupenya kundi hili kama nchi mwenyeji kitakwimu,
ingawa ubora wa FIFA si kigezo sana katika maandalizi kimbinu na kiufundi kwa maana nzima ya
maandalizi.
Kwenye mechi ya ufunguzi Urusi itakutana na Saudi Arabia ambayo ndiyo mechi pekee yenye
matumaini kwa asilimia 50 kushinda, ukiangalia ubora wa vikosi vya Uruguay ikiwa na akina Cavan na
Suarez huku Mohamed Salah akizidi kuonesha ubora wake na Liverpool.
Kundi B
Kwenye kundi hili ndimo alimo mfalme wa soka kwa sasa duniani, Christiano Ronaldo, na kikosi cha
Ureno kitakachofungua mechi za makundi na Uhispania, hii inasadikiwa kuwa fainali ya mwisho kwa
Ronaldo kutokana na umri wake.
Uhispania hawakuwa bora michuano ya mwaka 2014 nchini Brazil, hali iliyowafanya kushindwa kuvuka
hatua ya makundi hivyo inaleta changamoto kwa Ureno, Morocco na Iran. Morocco inahitaji kuwa makini
zaidi ikiwa mara yake ya kwanza tangu fainali za mwaka 1998.
Kundi C
Katika kundi hili, Ufaransa inapewa nafasi ya kupenya kutoka katika kundi hili kutokana na wachezaji
wenye viwango vizuri kama kiungo wa Manchester United, Paul Pogba, Oliver Giroud kutoka Arsenal
(Gunners) na Antoine Griezmann wa Atletico de Madrid. Wengine kwenye kundi hili ni Australia, Peru na
Denmark.
Peru imerudi kwenye michuano hii baada ya kutoshiriki kwa miaka 38 ikipitia njia ya mtoano. Endapo
Ufaransa itazichanga vyema karata zake kuna uwezekano wa kuingia hatua ya 16 bora.
Kundi D
Kundi hili nalo lina mfalme mwingine wa soka duniani, Lionel Messi, na kikosi cha Argentina wakiwa na
nchi za Croatia, Iceland na Nigeria. Kwa mtazamo wa karibu unaweza kusema Argentina wakiongozwa
na Lionel Messi wanaweza kupita kwa urahisi.
Lakini, hata hivyo, Iceland katika fainali za Euro mwaka 2016 waliing’oa England licha ya udogo wao, pia
hakuna asiyekumbuka maajabu ya Croatia mwaka 1998 nchini Ufaransa, hili ni kundi gumu lisilotabirika.
Kama hiyo haitoshi, Nigeria hivi karibuni ilicheza mechi ya kirafiki na Argentina na kuifunga 4-2, hivyo
licha ya kupewa nafasi ndogo kupenya lakini anaweza kusonga mbele katika kundi hili.
Kundi E
Hapa kuna mabingwa mara tano wa kombe hili “the selecao” Brazil, ikipewa nafasi kubwa kusonga
mbele. Hapa Serbia, Costa Rica na Uswisi wana kazi ya ziada kuizuia Brazil kuingia hatua ya 16 bora.
Brazil ndiyo iliyokuwa nchi ya kwanza kufuzu michuano hii na hivi karibuni chini ya kocha mzawa, Tite,
wamekuwa na kiwango bora sana, pia Neymar Jr kushindwa kuipa Kombe Brazil mwaka 2014,

anatarajiwa kama ‘key player’, kufuata nyayo za akina Rivaldo Borba Ferreira, Evengelista Cafu,
Ronaldinho Gaucho, Ronaldo De Lima na wengineo.
Kundi F
Kundi hili linalohesabiwa kuwa kundi la kifo lina bingwa mtetezi, Ujerumani akiwa na wakali wengine
kama Mexico, Sweden na Korea Kusini, nchi ambazo soka lao linakuwa kwa kasi na wamekuwa na
maandalizi mazuri kuelekea fainali hizi.
Ni dhahiri Ujerumani wanaweza kupenya kundi hili lakini Mexico siyo timu ya kubeza kwa
sababu walifikia hatua ya makundi fainali za mwaka 2014 nchini Brazil, pia Sweden ambao
walimwondoa Italia, wanashiriki fainali hizi tangu mwaka 1956.
Kundi G
Hapa kuna nchi za Ubelgiji, England, Panama na Tunisia, licha ya Ubelgiji kuwa bora kitakwimu, lakini
England wanapewa nafasi kubwa kusonga mbele, kutokana na maandalizi yao wakitengeneza kizazi
kipya cha soka cha akina Harry Kane.
Meneja wa England wa hivi sasa, Southgate, fainali za mwaka 1998 alikuwa mlinzi wa kati wa England
wakiwaadhibu Tunisia, hivyo atajipanga vema kulinda ‘legacy’ yake na taifa hilo kwa ujumla.
Kundi H
Hapa kuna Senegal, walioweza kufika hatua ya robo fainali mwaka 2002, Colombia, Japan na Poland
iliyo chini ya Lewandowsky, ni kundi ambalo kila timu ina uwezo wa kuvuka hatua ya makundi endapo
itakuwa na maandalizi mazuri.

By Jamhuri