Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa anahitaji uchunguzi kufanyika ilikubaini kama shirika la upelelezi la FBI lilijipenyeza kuchunguza kampeni zake kwa maslahi ya kisiasa.

Kupitia ukurasa wake wa tweeter,Trump amesema kuwa anahitaji kujua kama mtangulizi wake aliagiza kitu kama hicho kufanyika.

Katika ombi ambalo hii leo siku ya jumatatu Trump anataka kulitoa rasmi,linakuja kufuatia baada ya vyombo vya habari vya Marekani kudai kuwa FBI walikuwa na watu wao wa siri kwenye mikutano ya ndani ya Trump kwa lengo la kumchunguza.

Hadi sasa tayari kuna taarifa za kina za kiuchunguzi kuhusiana na mwenendo mzima wa kampeni zilivyoendeshwa.

Kwa siku ya jumapili Trump kupitia ukurasa wake wa Twitter alikuwa na mfululizo wa madai ya kukanusha na kudai hakuna ushahidi wowote wa kuzihusisha kampeni zake na Urusi.

Na ni kufuatia uchunguzi unaoendelea chini ya Robert Mueller hukusiana na jitihada za Urusi kuingilia uchaguzi wa mwaka 2016,kwa lengo la kuchagiza ushindi wa bwana Trump.

Gazeti la New York Times lilichapisha taarifa iliyodai kuwa FBI walituma mtu wao kufuatilia mwenendo wa kampeni za Trump mara tu walipopata taarifa za uwezekano wa Urusi kuingilia uchaguzi huo.

Hata hivyo vyombo vya kisheria vimegoma kutoa ushahidi majina ya maofisa waliohusika katika uchunguzi huo kwa kuhofia usalama wao.

Jambo jingine linalotarajiwa ni Trump kuagiza idara ya sheria ambayo inamvutano na FBI ili iweze kutoa nyaraka hizo za uchunguzi.

Mchambuzi wa BBC Antony Zurcher,anasema kuwa Robert Mueller anaonekana kupiga hatua katika uchunguzi wake,jambo ambalo lina muudhi Trump.

By Jamhuri