Achana na majina ya Sven van der Broeck wa Simba na Luc Eymael wa Yanga, tubaki na majina ya makocha wa hapahapa Afrika ili tuzungumze kitu kinachoeleweka. Hawa utawauliza tu nini kifanyike.

Maana ukizungumzia kocha kutoka Malawi, Zambia, Kenya, Uganda, Burundi au Rwanda ni kitu kitakachoeleweka kwa wengi, lakini ukienda Ulaya watabisha tu! Watasema wametuacha mbali. Makocha waoga? Ndilo swali unalopaswa kujiuliza. Hawataki kutoka kwenda nje ya Tanzania? Je, wana elimu ndogo? Au wanaumwa ugonjwa wa kupenda nyumbani? Unajiuliza maswali mpaka unakereka.

Hebu tuanze. Jamhuri Kihwelo alitangaza kuacha kufundisha soka na kujikita kwenye shughuli nyingine na kwa wapenda michezo haukuwa uamuzi mzuri hata kidogo. Julio, kama ajulikanavyo, ni mmoja wa makocha wazalendo wenye kuupenda mpira wa miguu kwa dhati kabisa. Kukatishwa kwake tamaa na madudu ya waamuzi wetu wazalendo ni kurudishwa nyuma kwa juhudi za makocha wengine ambao mafanikio yake, kwao ni chachu ya kutaka kufika mbali.

Kwa upande wa TFF hakuna lililoharibika, kwao si jambo lenye kuweza kuwanyima usingizi wanapomuona kocha ambaye amekuwa akitafuta elimu na ujuzi wa kufundisha kila kukicha, anaachana na ufundishaji wa soka.

Kocha anayekuwa tayari katika mazingira ya nchi hii kuteseka mikoani na wachezaji ambao hawalipwi mishahara kwa wakati, halafu akaamua kuachana na ufundishaji, ni pigo kwa makocha wengine wazalendo. Lakini cha ajabu ni kwamba kwa TFF hilo si pigo.

Tuje sasa. Masikitiko yanaongezeka pale ambapo ukweli Yanga inamtwaa Kocha kama George Lwandamina wa Zambia, huku Simba pia ikimtwaa Patrick Phiri, kutoka nchi hiyo hiyo. Makocha wawili kutoka Zambia wanakuja nchini kuongeza ubora wa soka letu na wanastahili kwa sababu nchi wanayotoka imeshawahi kubeba Kombe la Mataifa ya Afrika.

Ikiwa kocha kutoka Zambia anakuja kufundisha Tanzania, kwa nini ashindwe kufundisha Msumbiji, Angola, Zimbabwe na Namibia? Lakini kocha mzalendo ambaye kwa muda wote amekuwa akifundisha kwa sasa alitakiwa awe anafikiri kwenda angalau Afrika Kusini kufanya kazi, ila anafikia uamuzi wa kustaafu.

Makocha wa kigeni ambao mazingira ya wao kufanya kazi katika nchi zao ni rafiki wa taaluma zao, wanakuja Tanzania kuchuma fedha. Nadhani itatuchukua miongo kadhaa mpaka kuja kumuona kocha Mtanzania akiifundisha timu ya Ligi Kuu Zambia.

Kwa kuifundisha Yanga, George Lwandamina ameuzwa zaidi na ule wasifu wake. Ameitendea haki taaluma ya ukocha kama alivyofanya Mzambia mwenzake Patrick Phiri. Lwandamina na Phiri wamezitendea haki semina zote za ukocha walizozipitia nchini mwao Zambia mpaka kufikia hatua ya kuwa na heshima ya kazi zao kuwauza kimataifa.

Nini faida ya makocha wetu wazalendo kupewa semina nyingi za kukuza uwezo wao ikiwa mwisho wa siku wanakuja kukatishwa tamaa na madudu ya TFF hiyo hiyo ambayo imeshiriki kuwasomesha?

Kocha anayevunjika moyo anakuwa chanzo cha kuwanyong’onyesha makocha wengine wengi vijana ambao wanao uwezo wa kufundisha. Inatupasa tuone aibu kwa kuwa wepesi katika kuwapokea makocha wa kigeni huku tukiwapamba kwa kusifu mengi ambayo wameyafanya huko walikotoka. Tunacho kizazi cha makocha vijana wengi kama ambavyo Zambia inao wengi pia. Lakini wale wa Zambia wanakuja kufikia uwezo wa Lwandamina na Phiri na hawa wa kwetu wanakuwa ni makocha wa kuzunguka humu humu nchini.

Huyu George Lwandamina anaweza kabisa kuwa ni kocha mzuri, lakini kwa sababu ya Zambia kuwa ni nchi yenye kuwaandaa wengi kama yeye, anaweza kuwa mpita njia anayejifahamu kama alivyokuwa Patrick Phiri.

Akitoka hapa atakwenda Ethiopia na akiona mizengwe mingi anakwenda kwingineko. Nyuma yake wanakuwepo makocha vijana wa Zambia walio tayari kufuata nyayo zake, walio tayari kujiendeleza kimaarifa na walio tayari kwa kutokukatishwa tamaa na madudu ambayo labda yamo ndani ya FAZ.

Mchezaji kutoka Zambia afikirie kuchezea TP Mazembe na Mamelodi Sundowns kwanini kocha aliyemuibua kutoka mtaani asifikirie kufundisha klabu bora barani Afrika?

Kwenye siasa tunaweza kuwa katika ngazi sawa na Zambia, tukipigana ili TAZARA na TAZAMA zifanyiwe muundo wa kiuendeshaji kwa faida ya nchi mbili. Lakini kwenye soka hali ni tofauti kabisa, majirani zetu wanabakia katika viwango vya ubora wa wachezaji na makocha wakati sisi tunashuhudia kudorora kadiri siku zinavyokwenda.

Charles Boniface Mkwasa

Mholanzi Hans Van Der Pluijm alikuwa Yanga, ila alipoondoka alimchukua msaidizi wake, Charles Boniface Mkwasa, kuinoa timu ya Al Shaolla ya Saudi Arabia. Mwanzo ulikuwa mzuri.

Ni vigumu, lakini lazima tuhitaji ujasiri, tunapaswa kutoka hapa tulipo ila kuna hatua nyingi za kupitia kabla ya kufikia kile tunachotaka.”

Abdallah ‘King’ Kibadeni

Tunataka kutoka hapa tulipo, lakini kubwa zaidi lazima mafunzo yaendelee kutolewa na makocha wa kizazi cha sasa, kweli waamue kutoka, wapambane,” alisema kocha huyo wa zamani wa Simba.

By Jamhuri