Wastaafu wa kada mbalimbali serikalini wameitaka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) chini ya  Rais, Dk. Ali Mohamed Shein, kuonesha hati ya  Mungano wa Unguja na Pemba iwapo visiwa hivyo viliungana kisheria na mkataba kutambuliwa na Umoja wa Mataifa.

Uchunguzi wa JAMHURI umebaini hayo katika kongamano lililoitishwa na Jumuiya ya Wakulima na Wafanyakazi wastaafu Zanzibar lililofanyika katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari  huko Makunduchi, Mkoa wa Kusini, Unguja, wiki iliyopita.

Kongamano hilo likiwa chini ya aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Kati Unguja, Ali Hassan Khamis, katika utawala wa Awamu ya Sita Zanzibar chini ya Rais  mstaafu Dk. Amani  Abeid Karume, washiriki wameendelea kuhimiza visiwa hivyo kila upande kupata mamlaka yake kamili kama taifa.

Mjadala uliokuwa na mada mbili; za historia ya Zanzibar kuadhimisha Mapinduzi ya Januari 12, 1964 na ile ya  siasa na dini zilizowasilishwa na Ramadhani Nzori pamoja na Mwalimu Wahidi Kavishe. Mshiriki Zahra Abdulrazaq Mussa alisema kukithiri kwa mivutano na migongano ya kimawazo, kiitikadi na kiasili kunaweza kuleta hatari, hivyo umefika wakati jambo hilo kupatiwa utatuzi na  kuoneshwa hati ya Muungano ya visiwa hivyo.

Zahra alisema ikiwa wazee kutoka Pemba waliwahi kutaka himaya ya kisiwa chao na  mamlaka kamili, watu wenye asili ya Unguja nao wana wajibu wa kuvumiliwa ili kujitenga na wenzao wa Pemba.

Alisema mwaka 2001 kundi la wazee kutoka Pemba chini ya Mwenyekiti wao, Hamad Ali Mussa, aliyewahi kuwa Mbunge wa Ole, walifika Ofisi za Umoja wa Mataifa Dar es Salaam, wakitaka  kujitenga  na Unguja, hivyo  sasa ni zamu ya Unguja kupewa miliki ya kisiwa chao na  mamlaka kamili.

“Misuguano na mivutano  hii inatisha. Pemba na Unguja watu wake  siku moja wataingiana mwilini, njia pekee ni kila upande uwe na mamlaka, ioneshwe  hati ya Muungano kama ipo, tusilazimishane,” alisema Zahra.

Aidha, Zahra alisema umefika wakati wa mipaka ya  Unguja na Pemba itambulike, hati ya Muungano isomwe  kipengele kwa kipengele, tarehe na mwaka  wa kuungana ufahamike na kama hakuna kila upande uamue mambo yake.

Zahra ambaye ni mtoto  wa mwanasiasa mkongwe  Abdulrazaq Mussa Simai (Kwacha), alihoji masafa  kutoka Pemba hadi Unguja kuwa ni marefu yenye umbali kuliko Unguja na  Tanganyika (Mrima), hivyo umbali  huo unathibitisha si eneo moja.

Vuai Ali Haji, anayeishi Paje, Mkoa wa Kusini, alisema madai ya muda mrefu ya watu wa Pemba ni kutaka  Serikali yao, viongozi wa SMZ na SMT hawana haki wala wajibu wa kuwanyima haki hiyo huku akisema njia ya kiungwana ni wananchi hao kupewa mamlaka yao.

Alisema  ikiwa viongozi waliopo madarakani hawaoni  Zanzibar inakoelekea na tishio la kuvurugika kwa amani, utulivu na umoja kutokana na kukithiri kwa madai ya  watu wa  Pemba na Unguja, lolote linaweza kutokea.

“Uvumilivu una ukomo wake,  heri uwepo  Muungano wa Tanganyika na Unguja wa  Julius  Nyerere na Mzee Abeid Karume kuliko kuvutana kila kukicha, wapeni kisiwa chao, Waunguja tumechoka, hatuna  cha kupoteza kwa kutengana nao,” alisema Vuai.

Maryam Pandu anayeishi  Bwejuu akichangia, alisema waliopindua nchi kutoka mikononi mwa Sultan wa Oman, ndiyo wenye haki kulinda na kutetea Mapinduzi na kwamba  inashangaza kusikia  watu ambao hawakushiriki Mapinduzi Matukufu wakidai  nchi yao.

Mshiriki huyo alisema Mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 yalikuwa ni Mapinduzi ya Mungu kuwanusuru watu waliokandamizwa miaka mingi, hivyo yanapotokea  makundi ya ovyo ovyo  yakidhihaki na kukejeli, ni matusi na aibu kwa ASP na viongozi waliobaki.

Simai Jafari Bai, mkazi wa  Kijiji cha   Bambi, akichangia alisema Mapinduzi ya Zanzibar yalikuwa ni kwa ajili ya kukomboa watu wa Unguja ambako ndiko kulikokuwa shina la mateso, kubaguliwa,  kutumikishwa, kunyimwa ardhi, elimu na huduma za jamii na kwamba madhila hayo hayakuwasibu  watu wa Pemba.

Hata hivyo, Simai aliwaasa wananchi wa Unguja akiwataka waache kuuza ardhi na nyumba za umma  kwa matajiri, ambazo walipewa katika  utawala wa Rais Abeid Karume na  kuitaka SMZ izuie jambo hilo baada ya kuonekana watu wa Unguja kuwa ni madalali wa  kuuza utu na ardhi iliyo na rutuba.

“Iko hatari ya kutokea  vita ya ardhi kama Palestina na Israel. Wananchi wanauza ardhi na nyumba walizopewa na SMZ. Siku moja wanaouziwa watadai ni zao, wanyonge watakosa pa kuishi, kulima na maeneo ya kuzikana,” alisema Simai huku akishangiliwa.

Pia aliwatahadharisha wananchi wa Kisiwa cha Unguja kubaini mpango mkakati wa watu kutoka Pemba, wanaohamia kwa kasi Unguja na kusema bila ya tahadhari, Unguja itamezwa na Pemba kwa sababu  watu kutoka Unguja hawana dhamira ya kuishi Pemba.


By Jamhuri