Desemba 9, 2018 imeangukia siku ya Dominika, ni siku ya Bwana, sisi Watanganyika tumefanya kumbukumbu ya mwaka wa 57 wa Uhuru wa taifa letu. Ni fahari kubwa sana kwa sisi sote kukumbuka Desemba 9, mwaka ule wa 1961 tuliojikomboa kutoka mikononi mwa wakoloni Waingereza.

Kwa wazee kama Mhesheshimiwa Balozi Job Lusinde kule Dodoma, nafikiri inakuwa siku ya kumbukumbu ya namna ya kipekee. Huyu mzee wa miaka 88 sasa ndiye waziri pekee aliyehai na kuona maendeleo ya nchi kuanzia Serikali ya Awamu ya Kwanza ya Baba wa Taifa akiwa Waziri kuanzia Mei Mosi, 1961 tulipopata Serikali ya Madaraka ya Ndani – “Full Internal Self – Government” mpaka akaja kuwa Balozi, akastaafu na sasa anaona hii Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Magufuli ilivyobunifu na yenye uthubutu wa hali ya juu sana (very daring government).

Nimejaribu kumwelezea Mheshimiwa Rais Dk. Magufuli katika makala zangu kwenye JAMHURI matoleo Na. 374 na 375 zenye kichwa cha habari “Bravo: Rais Magufuli” na nikatia usemi ule wa Julius Ceasar – yule Empara wa Roma kwa maneno yale ya kilatini “veni, vidi, vici” baada ya kuhutubia lile kongamano pale Mlimani mwezi uliopita.

Novemba 29, 2018 nilibahatika kutembelea kule Soga, kituo kikuu cha ujenzi wa reli inayoitwa Standard Gauge Railway (SGR). Siyo masihala, pale ipo kazi au niseme kazi ya ujenzi imepamba moto kweli kweli. Baada ya kufurahia maendeleo ya wanavyofanya kazi hii, nikajirudia Dar es Salaam kwa kufuata barabara iliyopo sambamba na reli ile kuanzia hapo Soga mpaka Pugu, Dar es Salaam. Nimeona mengi ya kutia moyo, hasa vikosi (gangs) vya ujenzi sehemu mbalimbali vinavyochapa kazi. Siyo mchezo. Ni kazi kweli kweli.

Siku chache tu baada ya mimi kuzuru Soga, nikajionea kwenye runinga kuwa waheshimiwa wabunge wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii nao wameitembelea reli hii ya SGR kuanzia Dar es Salaam, Soga hadi Morogoro. Hapo nimefarijika sana maana nilikuwa najiuliza baada ya mimi kuona maendeleo yale pale Soga, vipi watoa uamuzi wa fedha bungeni hawaji kuona matumizi ya fedha zao? Kumbe nao walikuwa na azma hiyo hiyo ya kujionea maendeleo ya ile SGR.

Kama tunakumbuka vema Rais John Magufuli alizuru kituo cha Soga kuzindua kazi ya ujenzi wa hii SGR. Makamu wa Rais Bibi Samia Suluhu Hassan amejionea kwa macho yake kazi inayofanyika pale Soga. Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Kassim, Mbunge wa Ruangwa pia ametembelea Soga kuona kazi ilivyopamba moto.

Hata uongozi wa chama tawala kama Humphrey Polepole alifika pale hata akakubaliana na uongozi wa kambi ya Soga kuajiri vijana 100 wa Soga katika mradi huu wa reli ya kisasa.

Nikawa najiuliza mbona Mheshimiwa Spika Job Ndugai hajapazuru Soga naye akoleze bungeni umuhimu wa mradi wa reli yetu hii ya umeme? Basi, ninaomba sana. Mheshimiwa Spika, hata ile Kamati ya Bunge ya Fedha (sijui kama niko sahihi kama inaitwa hivyo) na Kamati ya Bunge ya Miundombinu nao watembelee mradi huu muhimu wajionee maajabu.

Kwanini nasema maombi namna hii? Wapo Watanzania mpaka leo hii hawaamini kama mradi huu wa reli ya SGR na ule wa umeme wa Stigler’s Gorge ita-materialize. Wengi hasa baadhi ya wanasiasa na wabunge wetu mimi ningesema wamekuwa ni “akina Tomaso”.

Mimi ninaandika kwa kusifia kazi nzuri niliyoona pale Soga katika mradi huu. Baadhi ya Watanzania naona bado wana shaka na mradi wenyewe. Hawaamini kama utakamilika. Watu namna hii tunawalinganisha na yule Mtume Tomaso, mmoja wa wale mitume Thenashara wa Bwana wetu Yesu enzi zile za Mayahudi kwenye utawala ule wa Rumi.

Tunasoma katika Injili ya Mtume Yohani Sura ile ya 20 maneno haya“… Ikawa jioni siku ile ya kwanza ya juma, pale walipokuwapo wanafunzi, milango imefungwa kwa hofu ya Wayahudi, akaja Yesu, akasimama katikati yao, akawaambia – “AMANI IWE KWENU…” Naye akisha kusema hayo akawaonyesha mikono yake na ubavu wake…” (Yoh. 20:19 – 20).

By Jamhuri