Na Dotto Kwilasa,JamhuriMedia,Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amemuapisha na kumtakia kheri Waziri Mkuu mpya wa Tanzania Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akimtaka kuepuka vishawishi vya ndugu, jamaa na marafiki na badala yake ajielekeze zaidi katika kuwatumikia Watanzania.

Rais Samia amebainisha hayo leo Ijumaa Novemba 14, 2025 katika hotuba yake muda mfupi baada ya kumuapisha Dkt. Nchemba Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, akimtaka kusimamia kikamilifu utekelezaji wa yale yaliyoahidiwa kwa watanzania wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu.

“Kwa umri wako mzigo huu ni mkubwa na vishawishi ni vingi kutoka kwa marafiki, ndugu, jamaa na wengine, nafasi yako hii haina rafiki, haina ndugu, haina jamaa- ni nafasi ya kulitumikia Taifa kwahiyo nikutakie kila la kheri katika utumishi wako.” Amesema Rais Samia.

Rais Samia amesisitiza kuwa muda ni mchache katika kutekeleza yale waliyoahidi kwa wananchi, akimtaka kusimamia vyema baraza la Mawaziri kwa kutumia vyema uzoefu wake katika Wizara ya fedha na kumsimamia vyema atakayekuwa Waziri wa fedha ili fedha zipatikane katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.

Dkt. Samia katika hatua nyingine leo mchana anatarajiwa kuzindua Bunge la 13 la Tanzania, akieleza kuwa katika hotuba yake ataeleza mwelekeo wa Serikali yake na vile vitakavyokuwa vipaumbele katika miaka mitano ijayo.