Na Munir Shemweta, WANMM MUHEZA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Leonard Akwilapo amewaongoza Mawaziri wenzake wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Ofisi ya Raisi Mipango na Uwekezaji katika kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.

Kikao hicho kimefanyika tarehe 18 Februari 2026 katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Muheza Mkoa wa Tanga ikiwa ni utekelezaji wa masuala yaliyojitokeza wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba.

Mawaziri hao ni Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa TAMISEMI na Dkt. Pius Chaya, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji ambao kupitia kikao hicho, kilichohusisha pia wataalamu, viongozi hao walipata fursa ya kuwahoji wananchi walioguswa na migogoro hiyo ya mashamba ya uwekezaji ambayo yaliyofutiwa umiliki mwaka 2016.

Mashamba hayo ni Azimio/ Kilapula Geiglitz, Bwembwera, Kibaranga, Kihuhwi, Lewa pamoja na Saguras yaliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Prof. Riziki Shemdoe (Wa pili kushoto) akizungumza katika kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.