Maafisa wa Marekani wamesema Wizara ya Mambo ya Nje imeidhinisha mauzo ya ndege za kijeshi na silaha zenye thamani ya dola bilioni 1.4 kwa UAE kuelekea ziara ya Rais Donald Trump wiki hii Mashariki ya Kati.

Maafisa kutoka idara ya usalama na Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani wamesema katika taarifa kuwa, mauzo hayo yanahusisha helikopta aina ya CH-47 Chinook na silaha nyingine ambazo “zitatumika kuunga mkono sera za kigeni na usalama wa Marekani.”

Wameongeza kuwa Umoja wa Falme za Kiarabu itatumia silaha na vifaa hivyo katika shughuli za uokoaji, kutoa misaada wakati wa majanga, misaada ya kibinadamu na operesheni za kupambana na ugaidi.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa Umoja wa Falme za Kiarabu ni mshirika muhimu wa Marekani katika kuimarisha uthabiti wa kisiasa na maendeleo ya kiuchumi katika eneo la Mashariki ya Kati.

Trump anatarajiwa kufanya ziara katika mataifa yenye utajiri wa mafuta ya Saudi Arabia, Qatar, na Umoja wa Falme za Kiarabu wiki hii kujadili mahitaji ya kidiplomasia kuhusu Gaza na Iran, pamoja na mikataba ya kibiashara kwenye sekta ya ulinzi, anga, nishati na akili mnemba.

Bunge la Marekani Congress lina siku 30 kuzuia mauzo hayo ya ndege za kijeshi kwa Umoja wa Falme za Kiarabu.