Balozi Hamad Khamis Hamad amekutana na Margarida Adamugu Talapa, Rais wa Bunge la Jamhuri ya Msumbiji kwenye Ofisi za Bunge hilo Jijini Maputo.

Wakati wa mkutano huo, Talapa alimpongeza Balozi Hamad kwa kuteuliwa kuiwakilisha Tanzania nchini Msumbiji na kumhakikishia kila aina ya ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake.

Aidha, alieleza kutambua ushirikiano na msaada wa Tanzania tokea wakati wa mapambano ya kutafuta Uhuru wa Msumbiji na jitihada zinazoendelea za kutafuta amani Kaskazini mwa Msumbiji.

Kwa upande wake, Balozi Hamad alimshukuru Mhe. Talapa kwa kukubali kukutana naye na alimhakikishia kila aina ya ushirikiano kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidugu na historia baina ya Tanzania na Msumbiji. Aidha, alishauri kuhusu umuhimu wa Mabunge ya nchi hizi mbili kuendeleza ushirikiano hasa baada ya Tanzania kumaliza Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba, 2025.

Mwisho, alieleza kwamba Tanzania itaendelea kushirikiana Serikali na Wananchi wa Msumbiji katika maeneo mbalimbali hususan utunzaji wa amani Kaskazini mwa nchi hiyo ambapo Majeshi ya Tanzania yanaendelea kusaidia kwenye mapambano dhidi ya vikundi vya kigaidi.