Rais wa Marekani Donald Trump amesema huenda akakutana na rais wa Urusi Vladimir Putin hivi karibuni kabisa.

Rais wa Marekani Donald Trump alikuwa akijibu swali aliloulizwa na waandishi habari katika ikulu yake ya White House mjini Washington ni lini atakapokutana na marais wa Ukraine na Urusi.

Kauli ya Trump kusema atakutana na Putin inafuatia kile ambacho rais huyo wa Marekani amekieleza kuwa ni mazungumzo yenye tija kubwa yaliyofanyika mjini Moscow kati ya mjumbe wake maalumu na rais Putin.

Mkutano huo unaotarajiwa kufanyika ulijadiliwa katika mazungumzo ya simu kati ya Trump na rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, ambayo kwa mujibu wa duru ya ngazi ya juu mjini Kiev yalimjumuisha pia katibu mkuu wa jumuiya ya kujihami NATO Mark Rutte na viongzi wa Uingereza, Ujerumani na Finland.

Trump hakutoa dalili zozote ni wapi mkutano wake na Putin utakakofanyika.