Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Dar

ASKARI 300 wameongezwa katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa ajili ya kuimarisha msako wa kuwatafuta na kuwakama wahalifu maarufu kwa jina la ‘Panya Road’.

Hayo yamebainisha leo Septemba 15, 2022 na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC), Amos Makalla alipokuwa akizugumza na wananchi wa Kata ya Zingiziwa mara baada ya kutembelea ujenzi wa barabara ya Chanika -Homboza.

Makala amesema kuwa msako wa kuwasaka wahalifu hao umeanza tangu jana na kuwaeleza wazazi ambao watapotelewa na vijana wao kuanzia leo Alhamisi wawatafute kwenye vituo vya Polisi au hospitali za wilaya.

Amsema kuwa inasikitisha sana kuendelea kufanyika kwa vitendi vya uhalifu katika mkoa huo huku wanaohusika wakiwa ni watoto ambao wazazi wao wapo na wengine hushindwa kushughulika nao.

“Hawa Panya Road ni watoto wetu na kama baadhi ya wazazi wameshindwa kuzungumza nao basi sisi tutashughulika nao na tayari tumemwaga askari 300 ili kuimarisha ulinzi katika Mkoa wa Dar es Salaam ,” amesema

Makala amesema kuwa kuanzia leo mzazi atakayebainika kupotelewa na mtoto afike katika hospitali kubwa za wilaya ikiwemo Muhimbili, Mwanyamala na Amana, Temeke” amesema Mwenyekiti huyo wa kamati ya ulinzi na usalama katika mkoa huo.

Hata hivyo Makalla amesema kuwa amesitikishwa sana na kifo cha mwanafunzin wa mwaka wa pili UDSM, Maria Baso (24),mkazi wa Kawe ambaye kundi la Panya Road walivamia nyumbani kwao na kuanza kuhalibu mali katika nyumba mbalimbali na kisha marehemu Maria kukatwa mapanga na kusababisha kupoteza maisha.

Pia ameongeza kuwa katika matukio ya Kawe na Tabata kuna vijana waliokamatwa kuhusiaka na matukio hayo ambao wametoka kutumikia vifungo vya miezi sita hadi mwaka mmoja jela.

By Jamhuri