Na Mussa Augustine.

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya( DCEA) imefanikiwa kukamata jumla ya kilo 16.643 za dawa ya kulevya zikijumuisha kilo 15.19 za heroin,gramu 655.73 za Cocaine na gramu 968.6e7 za Mathamphetamine zilizowahusisha jumla ya Watuhumiwa saba.

Hayo yamesemwa Desemba 7 2022 na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Kamishina Jenerali Gerald Kusaya wakati akizungumza na Waandishi wa habari nakubainisha kwamba ukamataji wa kilo 15.19 za dawa za kulevya aina ya Heroin zilizowahusisha watuhumiwa watatu ni mwendelezo wa oparesheni zilizopita nakwamba watuhumiwa hao ni Washirika wa Kambi Zuberi Seif na wenzake waliokamatwa na kilo 34.89 za heroin katika oparesheni ya mwanzoni mwa mwezi Novemba 2022.

Kamishina Jenerali Kusaya amewataja watuhumiwa hao watatu kuwa ni Suleiman Thabit Ngulangwa(36)mkazi wa Salasala,Sharifa Seleman Bakari(41) mkazi wa Maji Matitu Mbagala,Farid Khamis Said ( 22) mkazi wa Maji Matitu Mbagala ambao wote ni wakazi wa Dar es salaam.

Kamishna Jenerali Kusaya amewataja watuhumiwa wengine wanne ambao wamekamatwa wakiwa na gramu 655.75 za Cocaine na gramu 968.67 za Methamphetamine ambapo wamekamatwa wakiwa kwenye harakati za kufmsafirisha dawa hizo za kulevye kwenda nje ya nchi.

” Watuhumiwa hao wanne ni Hussein Rajab Mtitu ( 28) marufu kama Chodri Mohamedi mkazi wa Kibonde Maji Mbagala,Jaalina Rajab Chuma (31) maarufu kama Jaalina Mohan mkazi wa Tandika,Shabani Abdalallah Said( 36) mkazi wa Kilimahewa Tandika ambao wote ni Wakazi wa Dar es salaam,pamoja na Irene Dickson Mseluka (39) mkazi wa Ndala Mkoani Shinyanga,watuhumiwa wote wanaendelea kuhojiwa na watafikishwa mahakamani mara baada ya taratibu za kiupelelezi kukamilika” alisema.

Aliendelea kusema kuwa kutokana na kuimarika kwa udhibiti wa dawa za kulevya nchini wahalifu wa dawa za kulevya wamekuwa wakibuni mbinu mbalimbali ili kufanikisha uhalifu wao,nakwamba mamlaka hiyo iko macho na inaendelea kukabiliana na mabadiliko ya mbinu hizo.

” Tunashirikiana na Makampunu ya usafirishaji wa vifurushi ,vyombo vyote vya ulinzi na usalama na wadau wengine katika udhibiti na mapambano dhidi ya dawa za kulevya ili kukabiliana na mbinu mpya za usafirishaji na uuzaji wa dawa za kulevya,tunataka kuhakikisha tunakuwa na Tanzania isiyo na Madawa ya Kulevya” alisisitiza Kamishna Jenerali Kusaya.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi Mkuu huyo wa DCEA amewataka wasanii kuacha tabia ya kutunga nyimbo zinazohamasisha matumizi ya madawa za kulevya huku akisisitiza kuwachukulia hatua kali za kisheria wasanii wote watakao bainika wanahamasisha matumizi ya dawa za kulevya kupitia nyimbo zao.

By Jamhuri