“Hii kwetu ni kama kinyume kabisa, nitakuwaje na sahihi ya jiji na TABOA, bila kuwa na sahihi ya mwajiri wangu?  TABOA inamtambua mwenye basi na mimi natambuliwa na mwenye basi ambaye ni mwajiri wangu, kwahiyo naona si sahihi kuwa na kitambulisho ambacho hakina sahihi ya mwajiri wangu,” kilisema chanzo cha habari.

Ukikamatwa faini Sh 50,000

Kumekuwa na taratibu za kukamatwa kwa vijana wale wote ambao hawana vibali maalum. Baada ya kukamatwa watuhumiwa wamekuwa wakitakiwa kulipa faini ya Sh 50,000, ambayo kwa kwa namna moja ama nyingine haifahamiki kama ni dhamana au adhabu.

“Sisi ambao hatuna vibali maalum vya kuingilia pale getini, lakini tuna vitambulisho vya makampuni yaliyotuajiri ndiyo tumekuwa tukikumbwa na adha ya kukamatwa kila mara,

 

“Ukikamatwa faini ni Sh 50,000, pale polisi kituoni. Sasa hatujajua kama hii ni faini au ni dhamana. Ukikamatwa leo unalipa hiyo 50,000 unaachiwa, baada ya kama siku tatu unakamatwa tena unalipa tena 50,000, swali ni kwamba huu umegeuka mradi? Au ndiyo maana wameamua kutoa vitambulisho kwa watu wachache ili sisi tulionyimwa tuwe kama chanzo chao cha pesa? Alihoji dada mmoja ambaye alisema kuwa kukamatwa kwao limekuwa jambo la kawaida.

 

Afisa kutoka Chama Cha Kutetea Abiria (CHAKUA), Gervaz Rutaguzinda  alisema kuwa, kuna wakati abiria wanapata kero kutokana na kukamata baadhi ya makarani ambao wanadaiwa kutokuwa na vitambulisho maalum (gate passes).

 

“Utakuta karani anakuja kumuonyesha abiria gari ambayo anastahili kupanda ghafla anakamatwa, bila hata ya kusubiri kwanza akamalizana na huyo abiria, utaratibu huu kweli unawakera abiria,” Alisema

 

Ubabe wa viongozi

Vyanzo vya habari vinasema kuwa kumekuwa na vitendo vya ubabe na hasa pale mtu napokamatwa huwa hapewi nafasi ya kujitetea hata akifikishwa kituoni. Gazeti hili pia lilishuhudia kijana mmoja ambaye alikuwa ameingia ndani na pikipiki kumpokea ndugu yake akitiwa kashi kashi na askari wa ulinzi shirikishi kwa kumtishia kuwa atoke nje, lasivyo atampiga faini ya Sh 30,000. Kijana huyo aliponea chupuchupi baada ya mgeni wake kujieleza sana kuwa yule kijana alikuja kumpokea yeye.

 

“Kuna wakati kulikuwa na mkutano wa kwa ajili ya uzinduzi wa vitambulisho, kuna watu walitaka kuuliza maswali lakini chakushangaza watu walikataliwa wasiulize maswali,

 

“Mbali na hayo kumekuwa na ubabe mwingine ambao ukikamatwa pale kituoni bila kutoa Sh 50,000 kwanza uachiwi, hata kama kama mwajiri wako anakuja kukutambua,” kilisema chanzo cha habari.

Kauli ya SEUTA :

Shirika la Elimu ya Usafiri Tanzania (SEUTA) ni asasi isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa na kusajiliwa kwa sheria No. 24 ya 2002 kifungu cha 12 (2). Lengo kuu ni kuboresha mfumo wa huduma ya usafiri na usafirishaji wa abiria nchini pamoja na kuwajengea uwezo wa kutoa huduma hiyo kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali.

 

Mwenyekiti wa SEUTA, Hassan Mhita alisema kuwa wao kama wadau katika sekta ya usafirishaji wangefurahi kuoana kunakuwa na amani katika kituo cha mabasi cha Ubungo, kuliko kuendekeza mvutano na vitendo vinavyolalamikiwa kuwa ni vya unyayasaji.

 

“Ni vizuri wadau wakakaa pamoja wakajaribu kutafakari matatizo haya ambayo yanalamamikiwa na kutafuta ufumbuzi, na hasa suala hili la vitambulisho na ulinzi shirikishi yanaonekana kuleta mvutano zaidi na kuwaweka katika mazingira magumu baadhi ya watu ambao walishazoea kupata riziki yao pale kituoni,” Alisema Mhita

Alisema kuwa kwa asai hiyo kwa sasa imeanzisha utaratibu wa kuwapeleka makarani katika chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT) kusomea kozi fupi za  jinsi ya kuhudumia abria kwenye mabasi.

 

“Tumeingia makubaliano na NIT na tunataka hawa wanaotoka hapa chuoni ndiyo wapewe kipaumbele pale Ubungo kwani tayari wanakuwa na ujuzi kuliko kuwaweka wale ambao hawajui lolote,” alisema Mhita

Aidha Mhita alisema kuwa asasi hiyo iko katika mikakati ya kuboresha muundo wa polisi jamii katika kituo cha mabasi cha Ubungo kwa kuhakikisha kuwa kunakuwa na askari ulinzi shirikishi ambao watatambulika kuanzia katika mitaa yao.

 

Kauli ya Jiji la Dar es Salaam

Gazeti hili lilimtafuta Meneja wa kituo cha mabasi Ubungo, Juma Idd, kufanikiwa kukutana naye uso kwa uso, alisema kuwa yeye si msemaji bali kuna msemaji wa Jiji. Aidha alisema kuwa yeye huwa anapeleka taarifa zote za kituo hicho kila wiki makao makuu ya Jiji na kusema kuwa makao makuu wanajua kila kitu kinachoendela kituoni hapo.

 

Mwandishi wa gazeti hili aliwasiliana na Mkurugenzi wa jiji, Wilson Kabwe,  kwa njia ya simu ambaye alitoa maangizo kuwa mwandishi huyo arudi kwa meneja ndiye angeweza kuzungumuza masuala mbalimbali ya kituo hicho.

 

“Nenda pale Ubungo ukifika, nipigie niongee naye ili aweze kuongea na wewe” Amesema kwa njia ya simu.

Mwandishi alirudi tena kituoni hapo na meneja alitoa ahadi kuwa angeweza kukutana nae siku inayofuata kwani alikuwa nje ya ofisi.

 

“Sawa kesho tunaweza kuonana lakini kwanza nitakuwa na kikao kule Jiji, cha msingi tuwasiliane tu,” Amesema meneja huyo kwa njia ya simu

Kesho yake mwandishi wa habari alimkumbusha maneja huyo kwa ujumbe mfupi juu ya  kukutana, naye alijibu hivi; “Bado niko Jiji Makao Makuu Nangoja nionane na mkurugezi anipe hicho kibali cha kuzungumza.

Baadaye alituma ujumbe mwingine na kusema. “Kesho maana sikufanikiwa kumuona mkurugenzi”

 

Siku iliyofuata mwandishi alimtafuta tena Meneja huyo kupitia ujumbe mfupi wa simu. Baada ya saa kadhaa Meneja huyo lituma ujumbe mfupi kwenye simu na kusema kuwa “Niko Hospitali ya Lugalo ndiyo maana sijaweza kukujibu mapema. Sijafika kazini tangu asubuhi”

 

Mwandishi wa habari makala hii alituma ujumbe mfupi kwa Mkurugezi kumuelezea jinsi mchakato huo wa kumuona meneja ulivyoshindikana.

Hata hivyo mkurugezi huyo hakujibu lolote.

 

0783 106700


By Jamhuri