Na Abel Paul, Jeshi la Polisi Dar es Salaam

Jeshi la Polisi nchini kupitia Kikosi cha Afya na Hospitali ya CCBRT imetoa huduma za kibingwa kwa wananchi na Askari wa Jeshi la hilo wenye changamoto ya macho na mtoto wa jicho katika Hosptali Kuu ya Jeshi hilo iliyopo Kilwa Road jijini Dar es Salaam.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Kikosi cha Afya cha Jeshi la Polisi Afisa mnadhimu namba moja wa kikosi hicho daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake Kamishna msaidizi wa Polisi ACP Dr. Salum Luyeko amesema jeshi hilo linashirikiana na wananchi katika nyanja mbalimbali ikiwemo huduma za afya.

Dk Salum ameongeza kuwa Hosptali ya Jeshi hilo imekuwa na utaratibu huo kila mara ambapo wamekuwa wakitoa huduma tofauti tofauti kwa wananchi huku akiwaomba wananchi kufika hosptalini hapo kupata huduma za macho zinazotolewa na madaktari bingwa wa Jeshi la Polisi na CCBRT.

Kwa upande wake daktari bingwa wa macho kutoka hosptali kuu ya Jeshi la Polisi Kamishna msaidizi wa Polisi ACP Dr. Abdallah Mpallo amesema idadi kubwa ya wagonjwa wanaofika hospitalini hapo wanachangamoto ya mtoto wa jicho ambapo amewaomba kufika mapema kupata matibabu ili kuzuia uharibifu wa macho.

Nae Daktari bingwa wa magonjwa ya macho kutoka hospitali ya CCBRT Dr. Hamphrey Stanley amebainisha kuwa kliniki hiyo ilikuwa ya kupima uwezo wa kuona na kupima presha ya macho huku akiongeza kuwa wametoa huduma za ziada ikiwemo ushauri kwa wagonjwa wenye changamoto ya macho ili kuepuka matatizo makubwa yanayoweza jitokeza kwa kukosa ushauri mzuri.

Iddi Makame ambaye amepata huduma ya macho hosptali kuu ya Jeshi la Polisi kilwa Road ameshukuru hospitali kuu ya Jeshi hilo kwa kutoa huduma bora kwa wananchi waliojitokeza kupata huduma ya macho hospitalini hapo huku akiomba huduma hiyo kuendelea kutolewa mara kwa mara kwa wananchi wenye changamoto ya macho.

By Jamhuri