Kipigo cha Ihefu, kimewapeleka Yanga kwenye presha sahihi

Na Mwandishi wetu

Yanga wameagana na presha ya unbeaten na sasa wanaingia kwenye presha ya ubingwa. Kuna wakati presha ya unbeaten ilikuwa inawaondoa wachezaji kwenye focus ya ubingwa kiasi kwamba makocha walilazimika kuwakumbusha wachezaji na mashabiki kwamba wafocus kwenye ubingwa na sio unbeaten kwa sababu hakuna kombe la unbeaten. 

Mara kadhaa Kocha Msaidizi wa Yanga SC, Cedric Kaze, alisisitiza kwamba hawatafuti rekodi bali ubingwa. Baada ya kupoteza mechi ya jana ni kama Yanga wametua mzigo mzito vichwani mwao kwa sababu presha ya unbeaten ilikuwa haikwepeki. 

Baada ya kupoteza mechi ya jana naamini Yanga wataimarika na kuwa bora zaidi kwa sababu wameshaonja chungu ya kufungwa na wamesikia zomea zomea na kejeli za wapinzani zinavyokera baada ya kufungwa. Mayele na wenzake hawawezi kupoteza nafasi nyingi kizembe kama ilivyokuwa. 

Kipigo cha jana kitawaamsha Yanga lakini kinaweza kufanya timu nyingine zibweteke kwa kuanza kuiona Yanga ya kawaida kwa sababu wataanza kuamini kuwa wanaimudu Yanga kwa sababu tu imefungwa na Ihefu na hiyo itakuwa nafasi nzuri kwa Yanga kucheza kwa uhuru bila kukamiwa sana kama ilivyokuwa katika zama za unbeaten. 

Yanga baada ya kutoka sare na Al Hilal hapa Dar es Salaam kisha kipigo kule ugenini Sudan walizodolewa sana. Wakatoka CAFCL na kutua CAFCC ambapo walitoka sare nyumbani na Club Africain ambapo walizomewa pia na hiyo ikawa chachu ya ushindi wa Yanga nchini Tunisia na kelele za jezi nyeusi zilianzia huko. 

Zinazohusiana

 Yanga yachapwa na Ihefu FC 2-1

Kwa sasa Yanga inapumua. Imepoteza mechi moja huku ikiwa ina mechi moja mkononi ambapo wakifanikiwa kushinda wataongoza ligi Kwa tofauti ya point 3 dhidi ya Azam na 4 dhidi ya Simba SC. Presha ya ubingwa itawakamata kwa sababu sare au kupoteza kutawatoa katika uongozi wa ligi. Yanga hawatalala tena. 

Yanga wamepoteza mechi katika wakati ambao hawana presha ya ubingwa na labda iliwapa kurelux lakini baada ya kupoteza mechi wameingia katika presha ya ubingwa wakiwa na faida. Yanga itarejea na moto mkubwa zaidi kwa sababu wameingia katika presha sahihi kimashindano. Tutarajie unbeaten nyingine itakayokuja bila wao kuitafuta.