Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Dodoma

Rais wa Chemba ya Biashara,Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Paul Koyi amesema yeye ni kiongozi halali wa chemba hiyo kwa mujibu wa katiba.

Koyi ametoa kauli hiyo siku moja tu, baada ya baadhi ya wanachama wa chemba hiyo waliokutana jijini Dodoma kwa mkutano wa dharura wa Halmashauri Kuu ya TCCIA Taifa kwa siku moja ambao uliamua kumsimamisha kazi kutokana na mgogoro uliopo.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Koyi amesema amesikitishwa na uamuzi huo ambao aliuita ni batili kwa sababu hakina uamuzi wa kumsimamisha.

“Kikao kilichofanyika Dodoma jana (juzi), ni batili, mimi ni kiongozi halali ambaye nimechaguliwa na wanachama kwa kufuata katiba ya chemba yetu.

“Kikao hiki kilichokuwa chini ya ndugu Charles Chenza ambaye ni Mwenyekiti wa Chemba Mkoa wa Songwe, ni batili kwa sababu hakikufuata taratibu zetu katika uitishaji wa vikao, sikwenda kwa sababu haukuwa mkutano mkuu,”amesema.

Amesema tuhuma zote ambazo zimeelekezwa kwake hazitambui kwa sababu mpaka sasa hakuna mgogoro wowote ndani ya chemba.

“Nimesikitishwa mno na tuhuma zile ambazo ni feki, nchi yetu ina utawala wa sheria sasa inakuwaje inamhukumu mtu bila kumsikiliza, narudi tena kusema wanachama ndiyo wenye uamuzi si kikundi cha watu wachache,”amesema.

Amesema hana tatizo ndiyo maana amendeelea kuongoza chemba hiyo kwa mafanikio makubwa ndani ya Serikali ya awamu ya sita.

Rais wa Chemba ya Biashara Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Leo kujibu tuhuma za kuengeuliwa madarakani

“Hili ni kundi la watu wenye maslahi binafsi wanaotaka kutuvuruga, chemba iko imara na itaendelea kushirikiana na Serikali kutimiza majukumu yake ya kila siku na kazi yetu ni nzuri mno.

“Siwezi kukurupuka nafanya kazi za chemba kwa kufuata sheria ambazo ndiyo mwongozo wangu.

“Katika majukumu yangu, sihusiki kuajiri watumishi, kusaini cheki, sasa hizi tuhuma nahusika nazo kivipi,”alihoji Koyi.

Amesema ana kazi kubwa ya kuhakikisha anajenga taswira nzuri ya chemba, badala ya kukambatia migogoro isiyokuwa na maana.

Amesema anashangazwa mno kuona mkutano huo uliitishwa kwa siku mbili yaani Oktoba 28 na kumalizika Oktoba 30, mwaka huu, wakati katiba inasema lazima notisi ya siku 14 itolewe kwa wanachama.

Kikao kilichomsimamisha Koyi kilikuwa chini ya mwenyekiti wa kikao cha dharura, Charles Chenza, kilimtuhumu Koyi kwa matumizi mabaya ya madaraka.

By Jamhuri