Katibu Mkuu Wizara ya Nishati amefafanuwa kuwa changamoto ya mgao unatokana na umeme unaozalishwa kutokidhi mahitaji ya Watanzania wote.

Mramba ametoa kauli hiyo leo Februari 22, 2024 katika mkutano wa Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Zuhuru Yunus, unaohusisha viongozi mbalimbali na waandishi wa habari unaoendelea muda huu Ikulu Magogoni, Dar es Salaam.

Mramba amesema matatizo makubwa ya umeme wa Tanzania yako katika sehemu mbili ambayo ni uzalishaji na usambazaji.

Amesema uzalishaji usipokidhi mahitaji ndiyo kunakuwa na upungufu wa umeme unaopelekea mgao, kunakuwa na mgao kwa sababu umeme uliopo haukidhi mahitaji ya watu wote kwahiyo unalazimika kuwagawia hawa kwa muda huu na wale kwa muda huu, mahitaji ni makubwa kuliko umeme unaozalishwa.

“Mahitaji ya umeme nchini ni kati ya megawati 300 mpaka 400, mfano leo asubuhi tulikuwa na mahitaji ya megawati 304 ukiingiza megawati 235 (Kutoka kwenye mtambo wa Bwawa la Mwalimu Nyerere) utaona kwa kiasi gani itapunguza uhaba wa umeme.” Amesema Mramba.

By Jamhuri