Majaliwa asisitiza wabunge kushiriki michezo

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi kikombe cha ushindi wa jumla, Mwenyekiti wa Bunge Bonanza , Festo Sanga baada ya timu za Bunge kkuongozai  katika michezo mingi ya Bonanza hilo lilifanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari, John Merlin jijini Dodoma, Januari 28, 2023. Wa pili kushoto ni Spika wa Bunge, Dkt. Tulia Ackson na wa tatu kushoto ni Naibu Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo Jumamosi, Januari 28, 2023 ameshiriki Bunge Bonanza lililofanyika katika viwanja vya shule ya msingi na sekondari ya John Merlin ya jijini Dodoma ambapo ametumia fursa hiyo kuwasisitiza wabunge na wananchi wengine washiriki katika michezo ili kuipa miili yao nguvu na uwezo wa kutekeleza majukumu yao ya kikazi.

“…Michezo kwetu sisi wabunge ni muhimu zaidi kwa sababu inatufanya tuwe na afya bora zaidi na pia michezo inasaidia watu kukutana pamoja na kuimarisha undugu, kujenga urafiki pamoja na kukuza vipaji. Nampongeza Mheshimiwa Spika Dkt. Tulia Ackson kwa ubunifu huu wa kuanzisha Bunge Bonanza ambalo litakuwa linafanyika mara kwa mara.”

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo wakati akizungumza na wabunge, baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, Watumishi wa Bunge pamoja na maafisa wengine wa Serikali walio shiriki katika bonanza hilo. Amesema bonanza lingine kama hilo linatarajiwa kufanyika Juni 24, 2023.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitambulishwa na nahodha wa timu ya soka ya Bunge, ambaye pia ni Mbunge wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi kwa wachezaji wa timu hiyo  kabla ya mechi  kati ya Wabunge na Watumishi wa Bunge katika Bunge Bonanza kwenye viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari, John Merlin ya jijini Dodoma,

Kwa upande wake, Spika wa Bunge, Dkt. Tulia amesema Bunge Bonanza litakuwa linafanyika mara nne kwa mwaka lengo likiwa ni kuhamasisha wananchi umuhimu wa kushiriki katika kufanya mazoezi ili jamii iweze kuwa na afya bora zaidi.

Naye, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na Katibu wa Michezo wa Baraza hilo Mheshimiwa Nassor Salim Ali (Jazeera) ambaye amemuwakilisha Spika wa Baraza la Wawakilishi amesema baraza litaendelea kushirikiana na Bunge ili kudumisha undugu kupitia michezo pamoja na shughuli mbalimbali wanazozifanya. “Tunamshukuru Mheshimiwa Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kuendelea kudumisha Muungano.”

Awali, Mwenyekiti wa Bunge Bonanza, Mheshimiwa Festo Sanga alisema pamoja na mambo mengine bonanza hilo limeanzishwa ili kumuunga mkono Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ambaye amekuwa akiihamasisha jamii kushiriki katika kufanya mazoezi kwa ajili ya kuupa mwili afya na kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza.

Timu zilizoshiriki katika bonanza hilo ni timu ya Bunge na ya watumishi wa Bunge ambapo timu ya Bunge ilipata kombe la mshindi wa jumla baada ya kuishinda timu ya Watumishi wa Bunge katika michezo mingi. Michezo ni pamoja na mpira wa miguu, mpita wa wavu, mpita wa meza, mpira wa mikono, kuvuta kamba, kukimbiza kuku, kula chakula, kunywa soda, kuvuta kamba na kurusha tufe.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wachezaji wa timu ya soka ya Bunge na timu ya soka ya watumshi wa Bunge baada ya kukzikagua katika mechi ya Bunge Bonanza iliyofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari, John Merlin ya jijini Dodoma, Januari 28, 2023. Kulia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, George Simbachawene. (picha ns ofisi ys Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza katika Bunge Bonanza aliloliongoza kwenye viwanja vya Shule ya Msingi na Sekondari, John Merlin ya jijini Dodoma,