Rais wa Marekni, Donald Trump, ametishia kuiondoa nchi yake kutoka
katika Jumuiya ya Kujihami ya Mataifa ya Magharibi (NATO), iwapo
nchi wanachama wa Umoja huo ikiwamo Ujerumani hazitaongeza bajeti
ya ulinzi.
Amesema marais waliomtangulia walikuwa wakijaribu bila mafanikio
kuilazimisha Ujerumani na nchi nyingine tajiri kuongeza bajeti zao za
ulinzi dhidi ya Urusi bila mafanikio, na kuiacha Marekani ikilipa
mabilioni ya dola.
Amezitaka nchi tajiri zilizoko katika jumuiya hiyo hasa Ujerumani,
Ubelgiji na Hispania kutenga asilimia nne ya mapato ya nchi zao
katika bajeti ya ulinzi, akidai kwamba haiwezekani Marekani ikatumia
mabilioni ya dola kuiruzuku Ulaya.
Rais Trump amechukua msimamo huo wa kibabe kwa kuhoji thamani
ya jumuiya hiyo na kuongeza kuwa nchi yake haiwezi kukubaliana na
hali hiyo ya kuendelea kuziona nchi nyingine zikishindwa kuwasilisha
michango yao bila sababu.
Wakati hali ikiwa hivyo, nchi za Ulaya nazo zimemjia juu Rais huyo kwa
kuendelea kumkumbatia Rais wa Urusi, Vladmir Putin, pamoja na
shutuma nyingi zinazomkabili za kudaiwa kuingilia uchaguzi nchini
mwake.
Baadhi ya nchi wanachama na NATO, ikiwamo Uingereza,
imeishutumu Serikali ya Kansela Angela Merkel wa Ujerumani
kudhibitiwa kikamilifu na Urusi kutokana na maslahi ya kutaka bomba la
gesi asilia.
Zimedai Ujerumani imeanza kuilipa Urusi mabilioni ya dola kwa ajili ya
mahitaji yao ya nishati kutoka bomba la Urusi na kuishauri nchi hiyo
kujitafakari upya dhidi ya uamuzi wake huo.

Akizungumzia tuhuma za kushindwa kulipa michango kwa wakati, Rais
wa Ufaransa, Emmanuel Macron, aliwaambia waandishi wa habari
kwamba kila kitu kitakwenda kwa mujibu wa makubaliano ndani ya
Jumuiya hiyo ya NATO.
Hata hivyo, wakosoaji wa masuala ya kisiasa wamekuwa wakizitafsiri
kauli za Trump hasa za kuzilazimisha nchi za Ulaya ziongeze kiwango
cha bajeti ya ulinzi, zinatishia kuhujumu muungano huo ulioanzishwa
kwa lengo la kukabiliana na uchokozi wa uliokuwa Muungano wa
Sovieti.
Kansela Merkel ambaye alilelewa na iliyokuwa Ujerumani Mashariki,
ambayo ilikuwa chini ya utawala wa kikomunisti, amezungumzia jinsi
alivyowahi kushuhudia hali ya kudhibitiwa na Muungano wa Kisovieti,
amesema kamwe haitatokea nchi yake kuwa mateka wa nchi nyingine.
Amesisitiza juu ya mshikamano wa Jumuiya ya NATO katika kuamua
sera zao na kukanusha taarifa za nchi yake kuchukuliwa mateka na
Urusi kama anavyodai Rais wa Marekani, Donald Trump.
Waziri Mkuu wa Uingereza, Theresa May, pia ametoa wito wa
mshikamano miongoni mwa washirika wa NATO, na kuongeza
kuwa wakati Urusi inashirikishwa lazima suala hilo lifanyike chini ya
msimamo mmoja wa mshikamano na udhabiti katika NATO.
Ends

By Jamhuri