Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Khadija Nassir Ali, amewataka wananchi wa Mkuranga kuhakikisha wanalinda miundombinu ya gesi asilia iliyojengwa katika maeneo yao ili iweze kudumu na kuwanufaisha wananchi pamoja na taifa kwa ujumla.
Amesema ulinzi wa miundombinu hiyo ni jukumu la pamoja, huku akisisitiza wananchi kuendelea kuiunga mkono Serikali na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika utekelezaji wa miradi ya nishati safi.
Akizungumza katika bonanza la michezo na upimaji wa afya bure lililoandaliwa na TPDC Kisemvule , Mkuranga, Khadija amesema mradi wa usambazaji wa gesi asilia tayari umewezesha zaidi ya nyumba 500 kuunganishwa na huduma hiyo. Amesema bonanza hilo pia linalenga kuwakutanisha na kuwaunganisha wananchi wa Kisambule na Mkuranga kwa ujumla, sambamba na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi na ulinzi wa miundombinu.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amesema Mkuranga inajivunia kuwa miongoni mwa maeneo yanayonufaika na uwekezaji mkubwa katika nishati safi, akieleza kuwa matumizi ya gesi asilia yana mchango katika kutunza mazingira, kuokoa maisha ya wananchi na kurahisisha shughuli za kila siku majumbani.
Ameipongeza TPDC kwa kuichagua Mkuranga kutekeleza mradi huo na kuahidi kuwa Serikali ya Wilaya itaendelea kushirikiana na shirika hilo kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa na inatumika ipasavyo.
Khadija amesema matumizi ya nishati safi ni miongoni mwa vipaumbele vinavyoendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo wananchi wanapaswa kutumia fursa hiyo kwa manufaa yao na maendeleo ya taifa.
Amesema kuwa Serikali inalenga kuona uwekezaji mkubwa unaofanywa katika miundombinu ya nishati ukitoa matokeo chanya kwa wananchi, huku akiwataka wananchi wengi zaidi kujitokeza kutumia huduma hiyo kadri inavyofikishwa katika maeneo yao.
Kwa Upande wake Oscar Mwakasege Afisa Maendeleo ya Jamii Mwandamizi Kutoka Shirika la Petroli Tanzania (TPDC) amesema bonanza hilo na upimaji wa afya bure unalenga kuhamasisha ajenda ya matumizi ya Nishati safi ya kupikia na ulinzi na usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia huku akisema Katika Wilaya ya Mkuranga wameshawafungia Wananchi gesi alisilia nyumba 530 huku kwa Mwaka huu wa Fedha 2026/27 wanatarajia kuwafungia Huduma hiyo Wananchi zaidi ya 500 pia.
Kwa Upande wao Wananchi wa Kisemvule Mkoani Pwani Ally Rajabu na Sharifa Hassan wamelishukukuru Shirika la Petroli Tanzania (TPDC) kwa bonanza hilo na upimaji wa afya bure huku wakisema wamenufaika na gesi asilia wanayoitumia majumbani hivyo kutumia Nishati safi ukilinganisha na kipindi Cha nyuma walikuwa wanatumia chafu.




