Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesema Balozi Mstaafu Dkt. Willibrod Slaa, Mpaluka Nyangali maarufu Mdude na wakili Boniface Mwabukusi wamekamatwa kwa tuhuma za uhaini na sio kutokana na wao kukosoa mkataba wa uwekezaji bandarini kama inavyopotoshwa.

Kupitia taarifa aliyoitoa katika ukurasa wake wa mtandao wa twitter, Waziri Nape amesema, hakuna mtu yeyote ambaye amekamatwa wala hatakamatwa kwa kukosoa tu mkataba wa bandari au mradi, mpango, mpango au sera yoyote ya serikali.

Vilevile amesema, kauli kuhusu kukamatwa kwa watu hao zimechanganya mambo mawili tofauti ambayo ni mjadala wa kitaifa unaoendelea kwa uwazi kwa sasa nchini Tanzania kuhusu mapendekezo ya uwekezaji wa bandari kwa upande mmoja, na suala la sheria kwa upande mwingine.

Akielezea uhalisia wa kukamatwa kwa watatu hao Waziri Nape amesema,

“Watu hao watatu walikamatwa na Polisi kwa kutoa vitisho vya uhalifu hadharani, ambavyo ni pamoja na kutaka kupinduliwa kwa nguvu kwa serikali. Watuhumiwa hao ambao baadhi yao walitaka hadharani kuhamasisha wananchi kubeba silaha dhidi ya jeshi la polisi Tanzania, walikamatwa ili kutuma ujumbe mahususi wa kuwazuia wahalifu wengine kufanya makosa ya jinai”

Kufuatia hilo Waziri Nape amebainisha kuwa,
Kukamatwa kwao hakuzuii kwa vyovyote vile uhuru wa kujieleza nchini Tanzania, bali ni sehemu ya utekelezaji wa sheria ili kuzuia machafuko ya kijamii yanayoweza kutokea kutokana na wito wa uasi dhidi ya serikali iliyochaguliwa kidemokrasia.

Akizungumzia moja ya kauli za Shirika la Kimataifa la Kutetea Haki za Binadamu kuhusu sakata la kukamatwa kwa watu hao, Waziri Nape ameeleza.

“Moja ya kauli za hivi majuzi zaidi kutoka kwa shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu limeamua kupotosha ukweli kwa nia mbaya kwa kudai kimakosa kwamba washukiwa walikamatwa kwa kukosoa tu mpango wa bandari kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE)” alisema Waziri Nape na kuongeza kuwa.

“Watu binafsi, makundi, asasi za kiraia, wanataaluma, vyombo vya habari, viongozi wa dini, vyama vya siasa na taasisi wanaendelea kujadili kwa uhuru masuala ya kitaifa na kukosoa msimamo wa Serikali bila vitisho wala kukamatwa. Hivi sasa vyama vya upinzani vinafanya mikutano ya hadhara kwa uhuru nchini kote kukosoa mkataba wa bandari na sera nyingine za Serikali jambo ambalo hawakuweza kulifanya miaka michache iliyopita kabla ya utawala wa Rais Samia Suluhu Hassan kuingia madarakani”

Tangu kukamatwa kwa Balozi Dkt. Wilbrod, Mdude Nyagali na Wakili Boniface Mwabukusi watu mbalimbali wamekoa wakitoa maoni yao kuhusu sakata la kukamatwa kwao, miongoni mwao ni wadau wa haki za binadamu ambao wamelitaka jeshi la polisi kuwaachia kwa kile kilichodaiwa kuhusianishwa na ukosoaji wao katika mkataba wa ushirikiano wa kiuchumi na kijamii kati ya Serikali ya Tanzania na Dubai (IGA).

By Jamhuri