Rais wa Uturuk Recep Tayyip Erdogan ameitaka Saudia kutoa ushahidi kuhusiana na mwandishi wa habari aliyepotea kwamba alitoka nje ya majengo ya ubalozi wao mjini Istanbul.

Mwandishi huyo raia wa Saudia Jamal Khashoggi kwa mara ya mwisho alionekana katika jengo hilo la ubalozi wiki iliyopita.Hapo jana Rais Trump alielezea kusikitishwa kwake kutokana na kutoweka kwa mwandishi huyo.

Uturuki imeomba kufanya uchunguzi ndani ya majengo hayo ya ubalozi,kwa madai kuwa Khashoggi aliuawa ndani ya majengo hayo kwa mjibu wa taarifa za vyombo vya habari.

Siku ya jumapili wachunguzi kutoka Uturuki walisema wana uhakika kuhusiana na kuuawa kwa mwandishi huyo na kwamba aliuawa na watu 15 kutoka Saudia ambao wanadaiwa waliingia nchini humo wiki iliyopita.

Hakuna ushahidi uliowasilishwa.Mwana Mfalme Mohammed bin Salman awali alisema maofisa wa uchunguzi wanaruhusiwa kuingia katika majengo ya ubalozi wao nchini humo kupeleleza akisistiza hakuna jambo baya lililotendeka.

Khashoggi alikuwa akiishi Marekani ambako alikuwa akiandikia gazeti la Washington Post huku maoni yake yakionekana kuwa ni mmoja wa wakosoaji wa serikali ya Saudia.Gazeti hilo limesema kuwa Marekani inahitaji majibu kutoka Saudia.

Jamal Khashoggi alienda ubalozini hapo kwa leo kufuatilia vibali vya ndoa kati yake na mchumba wake raia wa Uturuki , Hatice Cengiz kufuatia kuvunjika kwa ndoa yake ya awali.

By Jamhuri