Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Dodoma

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amesema, Wizara ya Afya kwa kushirikiana na vyama vya kitaaluma inatekeleza Mkakati wa kuwajengea uwezo watumishi wa vituo vya huduma za Afya kuanzia ngazi ya Zahanati hadi hospitali za Taifa katika eneo la utoaji ganzi/nusu kaputi na upasuaji kwa usalama kwa kuzingatia miongozo.

Dkt. Mollel amesema hayo wakati akijibu swali la Christina Christopher Mnzava (MB) katika Mkutano wa 9 kikao cha kwanza cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jijini Dodoma.

Amesema, ufuatiliaji wa vifo vitokanavyo na uzazi uliofanywa na Wizara ya Afya kuanzia mwaka 2018 hadi 2021 umeonesha kuwa vifo ambavyo vilisababishwa na matatizo ya dawa za ganzi/nusu kaputi na upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni ni 58 (3.3%) mwaka 2018, vifo 80 (4.8%) mwaka 2019, vifo 65 (4.0%) mwaka 2020, na vifo 65 (4.1%) mwaka 2021.

Aidha, Dkt. Mollel amesema, Sababu kuu za vifo hivi ni 4 ambazo ni ajali ya dawa za ganzi/nusu kaputi, kupoteza damu wakati au baada ya upasuaji, tatizo la damu kuganda na maambukizi ya bakteria baada ya upasuaji.

Akijibu swali la nyongeza kuhusu mikakati ya Serikali ya kutatua changamoto hiyo Mhe. Dkt. Mollel amesema, kupitia mpango wa Serikali wa “Samia Health Super Specialisation Programme.” huku jumla ya Bilioni 8 zimetolewa na Mhe. Rais Samia, Serikali kupitia Wizara ya Afya imelenga kusomesha Wataalamu wa fani za kibingwa na kibingwa bobezi 339, huku 136 wakipata mafunzo nje ya nchi na Wataalamu 3. Huku akisema kuwa,

Ameendelea kusema kuwa, Katika utekelezaji wa Mpango wa mafunzo kwa kipindi cha miaka miwili (2020/21 na 2021/22) Wizara imefanikiwa kusomesha wataalamu bingwa 524 ambao wanaendelea na masomo kwenye vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi, ambao ndani yao wapo Wataalamu wa usingizi.

Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amesema, Serikali imepanga kununua magari ya kubebea wagonjwa (Ambulance) 663 yatayosaidia kupunguza vifo vya Wajawazito.

Amesema kuwa, kwa mwaka huu (2022) Serikali imejenga vitu vya afya 238, ikiwa ni mkakati mwingine wa Serikali katika kukabiliana na changamoto ya vifo vinavyotokana na uzazi.

By Jamhuri