SUMAYE: SINA MPANGO WA KURUDI CCM, AWATAJA JPM, JK NA MKAPA

KUTOKANA na kuibuka kwa wimbi la baadhi ya wanasiasa hapa nchini kuhama vyama vyao, Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Frederick Sumaye ambaye ni kada wa Chadema amefunguka na kusema kuwa hana mpango wa kurudi Chama Cha Mapinduzi (CCM) alikokuwa zamani kwani yeye yupo upinzani ili kukipa changamoto chama tawala.

Sumaye ameyasema hayo leo Ijumaa, Januari 5, 2017, ambapo amesema alikihama chama hicho kwa sababu anataka ifike mahali ambapo Chadema kitakuwa na nguvu kama kilivyo CCM na kuongeza kuwa anawapenda Marais wote wa walioiongoza Tanzania.

“Kwangu mimi suala la kurudi CCM hapana! tunachojenga ni demokrasia, sina chuki na CCM, sina chuki Rais John Magufuli, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, Rais Mstaafu Benjamin Mkapa wala uongozi.

“Rais Magufuli akifnya vizuri katika kupambana na ufisadi, kusimamia demokrasia na uchumi, mambo yote mhimu atakuwa ameyafanya yote ya msingi, hayo yatanifanya nimpe changamoto zaidi asirudi nyuma. Kwa sasa CCM wanajitahidi kufanya vizuri kwa sababu sisi wapinzani tunawakumbusha,” alisema Sumaye