Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imefaulu kuendesha kazi ya Vitambulisho vya Taifa kwa umakini mkubwa.

Hadi sasa imeweza kugawa vitambulisho kwa wabunge, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar na watumishi wa umma, mara baada ya uzinduzi wa Mfumo wa Usajili na Utambuzi wa Watu na Utoaji wa Vitambulisho vya Taifa, ulipozinduliwa na Rais Jakaya Kikwete Februari 7, 2013.


Vitambulisho vya aina hii vinaweza kutengenezwa kwa aina tano ya teknolojia duniani, ambazo ni Smart Card, Magnetic Stripe, Magnetic, Optical, na Plastic.  Katika aina hizo, Smart Card ndiyo aina bora kuliko aina nyingine zote kwa ubora duniani. Ndiyo teknolojia ambayo NIDA imeichagua na imeridhiwa na wadau mbalimbali, wakiwamo waheshimiwa wabunge.


Smart Card, pamoja na faida nyingine nyingi, uzuri wake ni kwamba ina:-

1.      Uwezo mkubwa wa kutunza

taarifa,

2.      Uwezo wa kutumika katika

mifumo mingi

3.      Usalama mkubwa wa kutunza taarifa za mtu

4.      Uwezo mkubwa wa kusomwa na vifaa maalum tofauti tofauti kwa matumizi tofauti              (card reader)

 

Kutokana na faida nyingi na matumizi yanayokusudiwa ya teknolojia hii ya Smart Card, Serikali, kupitia NIDA, inajenga Mfumo wa Usajili na Utambuzi wa Watu, ambao utakuwa na taarifa nyingi za kibinafsi na kibaiolojia za mwombaji.


Lengo kubwa ni kuwa na Daftari Kuu la Utambuzi na Usajili wa watu, ambalo litawasiliana na mifumo mingine ya Serikali kwa madhumuni ya kubadilishana taarifa na hatimaye kutoa vitambulisho kwa watu wote waliosajiliwa.


“Naomba niwahakikishie kuwa teknolojia iliyotumika katika utengenezaji wa vitambulisho vya Taifa, ni ya hali ya juu sana katika vitambulisho duniani na hapa Tanzania. Teknolojia hii ni ya ‘Contactless Smart Card’ ambapo ndani yake kuna contactless chip (chip zisizoonekana kwa macho) yenye uwezo wa KB (Killobites) 80,” amesema Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Dickson Mwaimu.

 

Kwa sasa taarifa zilizohifadhiwa katika Kitambulisho cha Taifa, na ambazo mtumiaji anaweza kuzisoma kupitia kifaa maalumu  (card reader), ni taarifa binafsi za mwombaji, taarifa za kibaiolojia (alama za vidole na picha), anuani ya makazi na posta,  pamoja na taarifa za viambatanisho vya mwombaji alivyowasilisha wakati wa usajili.


“Hizi ni taarifa chache kati ya nyingi ambazo bado zinaweza kuhifadhiwa katika kitambulisho cha mwombaji,” anasema Mwaimu.


Serikali iliamua kutumia teknolojia ya Smart Card na kuweka taarifa chache sehenu ya juu ya kitambulisho kwa lengo la kutambua picha, uraia, jinsi, nambari ya kitambulisho, na mwaka wa kuhuishwa kitambulisho chake kwa lengo la kutambua mwenye kitambulisho kama kikipotea.

By Jamhuri