Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Bagamoyo

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA),imedhamiria kufanikisha maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kufanya mageuzi makubwa ya uchumi wa nchi kutoka daraja la tatu kwenda kwenye nchi zenye uchumi wa daraja la pili.

Hayo yamebainishwa leo Oktoba 13, 2022 na Mkurugenzi Plasduce Mbossa katika kikao kazi na wahariri kilichofanyika Bagamoyo Mkoa wa Pwani na kuhudhuriwa na watendaji mbalimbali wa TPA.

Mkurugenzi Plasduce Mbossa akizungumza katika kikao kazi na wahariri kilichofanyika Bagamoyo Mkoa wa Pwani na kuhudhuriwa na watendaji mbalimbali wa TPA.

Amesema kuwa TPA inataka kuzifikisha bandari zake kwenye kiwango cha juu na cha kisasa kwa kuziunganisha na shughuli za biashara ya kitaifa na kimataifa.

“Uwepo wa bandari zenye uwezo mdogo na ufanisi wa chini ni kikwazo kikubwa kwa shughuli za uzalishaji na biashara ambacho kinaongeza gharama za huduma za bandari ambazo zinaishia kulipwa na walaji ambao ni wananchi wa kawaida wakati wa kununua huduma na mahitaji yao ya kila siku.

“Katika hili bandari hazipaswi kuwa na gharama kubwa za utoaji wa huduma zake kwa sababu haijapewa jukumu la kisheria la kukusanya mapato kuwa na bandari zenye ufanisi na manufaa kwa mwananchi mmoja mmoja na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Amesema kuwa TPA iko tayari kuhakikisha dira ya Serikali inatekelezwa kwani itakuwa ni hatua muhimu katika kuzifikia nchi zenye uchumi wa daraja la kwanza.

Mbossa amesema kuwa kipimo cha maendeleo ya bandari zetu nchini ni bandari za mwambo wa Pwani hususan bandari ya Dar es Salaam ambayo imekuwa tegemeo la nchi yetu na nchi jirani za Zambia,JaMhuri ya kidemokrasia ya Congo, Burundi, Rwanda, Malawi na Uganda

“Pamoja na kuwa tegemeo letu, bado kuna maboresho ya miundombinu na ya kiutendaji yanayopaswa kufanyika katika bandari zetu zote ili ziweze kuwa lango la biashara ya kitaifa na kimataifa” amesema.

Baadhi ya wahariri wakiwa kwenye mkutano

Mkurugenzi huyo amesema kuwa hivi sasa Serikali ya Awamu ya Sita, inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya uboreshaji wa bandari na ujenzi wa bandari mpya ili kuongeza uwezi kabla ya mahitaji.

Mbossa amesema kuwa kupitia maboresho yanayoendelea kutekelezwa , uwezo kuhudumia shehena katika bandari za Dar es Sakaam, Tanga na Mtwara unatarajiwa kufikia jumla ya tani milioni 27.5 ifikapo mwaka 2024/25 wakati matarajio ya shehena ni jumla tani milioni 26.1 ifikapo mwaka huo sawa na asilimia 94.9 ya uwezo wa bandari zetu za mwambao utakaokuwepo.

“Kutokana na matarajio ya shehena kuwa karibu na uwezo wa juu wa bandari zetu, tunapaswa kuanza kuandaa na kutekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi wa bandari za Bagamoyo katika Mkoa wa Pwani, Chongoleani katika Mkoa wa Tanga na Kisiwa-Mgao katika Mkoa wa Mtwara ili kuongeza uwezo wa bandari zetu.

“Vilevile kwa upande wa bandari za maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa, tumeboresha bandari zilizokuwepo na kujenga zingine mpya ikiwa ni pamoja na bandari ya Nyamirembe, Lushamba, Ntama za ziwa Victoria, Karena na Kagunga za ziwa Tanganyika na tumefanya maboresho ya bandari za Kiwira na Itungi za ziwa Nyasa,’ amesema.

Amesema kuwa Serikali kupitia mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), imekamilisha mpango kabambe wa uendelezaji wa bandari za Tanzania kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2022 hadi 2045 kwa lengo la kuziboresha ili kuendana na matarajio ya ongezeko la shehena na kufikia ufanisi unaotakiwa.

“Serikali inatakiwa kuwekeza katika miundombibu, ununuzi wa mitambo, mifumo ya uendeshaji wa bandari, kuboresha uendelezaji, usimami na uendeshaji wa bandari,” amesema.

By Jamhuri