Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak amepigwa faini kwa kutokufunga mkanda akiwa ndani ya gari lililokuwa katika mwendo.

Waziri Mkuu huyo ametozwa faini mara baada ya kujirekodi video akiwa ndani ya gari bila kufunga mkanda na kuituma katika ukurasa wake wa Instagram ambapo mamlaka zimebaini na kumchukulia hatua.

Sunak amekubali kulipa faini hiyo lakini pia ameomba radhi kwa kitendo hicho.

“Nakubali kabisa kwamba hili ni kosa, pia niombe radhi, na niko tayari kulipa faini.”amesema Sunak.

Waziri mkuu huyo alijirekodi video hiyo kupitia simu yake alipokuwa ndani ya gari katika mji wa Lancashire ulioko Kusini mwa Uingereza.

Sunak atatakiwa kulipa faini ya £100 sawa na Sh. 289,283 hadi £500 sawa na Sh. Milioni 1.4 kwa mujibu wa sheria za nchi hiyo

Mamlaka zinasema, kwa mujibu wa sheria za Uingereza mtu yeyote anayekamatwa kwa kosa la kutokufunga mkanda wa gari makusudi na mkanda huo ukiwepo basi atatozwa faini ya £100 sawa na Sh 289,283 na £500 sawa na Sh.Milioni 1.4 endapo shauri litafikishwa mahakamani.

Uingereza wamejitanabaisha kwa kusimamia na kufuata sheria zao bila kujali mamlaka au madaraka ya mtu.

Hata hivyo sunak siyo kiongozi wa kwanza mwenye wadhifa kama wa kwake kuwahi kukutwa na hatia kwa uvunjifu wa sheria.

Mnamo mwezi June 2020 aliyekuwa Waziri Mkuu wa uingereza kabla ya mtangulizi wa Sunak, Liz Trus aliyedumu kwa siku 21 madarakani na kujiuzuru , Boris Johnson naye alishtumiwa vikali kwa uvunjifu wa sheria za Karantini wakati wa kipindi cha UVIKO-19 kwa kile kilichodaiwa alifanya sherehe katika makazi yake huko Downing Street jambo lililozua mijadala mikali na kuibua hisia za wengi.

By Jamhuri