Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Tanga

Mchezo wa riadha watu wazima wenye umri wa miaka 50-59 umekuwa kivutio katika Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara za Serikali, Wakala na Mikoa (SHIMIWI) inayoendelea jijini Tanga.

Usemi wa “Yake ni dhahabu” umejidhihirika katika viwanja vya Shule ya sekondari ya Ufundi Tanga kwenye mashindano ya SHIMIWI ambapo watu wazima wenye umri wa miaka 50-59 wamechuana vikali kuonesha makali yao katika mchezo wa riadha mbio za Mita. 100 wanaume na wanawake.

Katika mbio hizo kwa Juma Chikuku kutoka Wizara ya Kilimo ameshika nafasi ya kwanza na kuwaacha Sulemani Juma kutoka Hazina ambaye ameshika nafasi ya pili na nafasi ya tatu kwenda kwa Charles Kulila kutoka RAS Mara na kwa upande wa wanawake nafasi ya kwanza imeenda Melania Kapungu kutoka RAS Arusha, nafasi ya pili imeshikwa na Anitha Kihiyo kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na nafasi ya tatu imekwenda kwa Salome Makubi kutoka Wizara ya Maji.

Mshindi wa kwanza wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara za Serikali, Wakala na Mikoa (SHIMIWI) katika mchezo wa riadha mbio za Mita 100 kwa watu wazima wenye umri wa miaka 50-59 kwa wanawake Melania Kapungu kutoka RAS Arusha akimaliza mbio hizo katika Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Tanga Oktoba 10, 2022 yaliyofanyika jijini Tanga

Kwa upande wa awtumishi wengine mchezo huo pia umerindima kwa wanamichezo kuoneshana makali yao katika mbio mbalimbali ikiwemo Mita 100, 200, 400, 1500 pamoja na mbio za Mita 100 kupokezana vijiti michezo yote ikishirikisha wanaume na wanawake,

Mshindi wa kwanza katika Mita 100 wanawake ni Anitha Brown kutoka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, nafasi ya pili imekwenda kwa Furaha Kaboneka kutoka Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi huku nafasi ya tatu imekwenda kwa Jamila Mkomwa wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi) wakati kwa upande wa wanaume kwenye mbio hizo nafasi ya kwanza imekwenda kwa Baraka Mashauri kutoka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi), nafasi ya pili imekwenda kwa Martine Zulumo kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia huku nafasi ya tatu ikienda kwa William Valentino kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

shindi wa kwanza katika mbio za mita 100 kwa Baraka Mashauri kutoka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi) akimaliza mbio hizo ambazo ni sehemu ya mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara za Serikali, Wakala na Mikoa (SHIMIWI) yaliyofanyika katika Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Tanga Oktoba 10, 2022 yaliyofanyika jijini Tanga.

Mbio nyingine zilizochezwa ni Mita 400 wanaume na wanawake, kwa upande wa wanawake nafasi imekwenda kwa Mastura Kaiza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi), nafasi ya pili imekwenda kwa Emerisiana Mtimbi kutoka RAS Pwani na nafasi ya tatu imekwenda kwa Mary John kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati kwa upande wa wanaume katika mbio hizo nafasi ya kwanza imekwenda kwa Aidan Adrian kutoka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi), nafasi ya pili imekwenda kwa Innocent Mbizo kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) wakati nafasi ya tatu ikienda kwa Mussa Himapande kutoka Wizara ya Kilimo.

Mwanariadha Anitha Bown wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ameibuka kidedea katika mbio za mita 200 wanawake akishika nafasi ya kwanza, akifuatiwa na Naomi Dominic wa Wizara ya Maji na watatu ni Neema Manyama wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi); wakati kwa upande wa wanaume Martin Zalumo wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ametwaa media ya dhahabu, akifuatiwa na Baraka Mashauri wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi), na watatu ni Omar Mwenda wa RAS Shinyanga.

Katika mbio za mita 1,500 wanaume mwanariadha wa kimataifa Elibariki Buko wa Wizara ya Maliasili na Utalii ametwaa ubingwa akifuatiwa na Joseph Kachala wa Wizara ya Afya na watatu ni Eliud Kitwila waWizara ya Mifugo na Uvuvi; wakati kwa upande wa wanawake Nyamiza Ndibalema wa Wizara ya Madini ya ameibuka bingwa akifuatiwa na Scolastica Halisi wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi) na watatu ni Johaness Sarakikya wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mshindi wa kwanza wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara za Serikali, Wakala na Mikoa (SHIMIWI) katika mchezo wa riadha mbio za Mita 100 kwa watu wazima wenye umri wa miaka 50-59 kwa wanaume Juma Chikuku kutoka Wizara ya Kilimo akimaliza mbio hizo katika Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Ufundi Tanga Oktoba 10, 2022 yaliyofanyika jijini Tanga.

Wakati huo huo michuano ya riadha imehusisha pia mbio za Mita 100 kupokezana vijiti wanaume na wanawake ambapo ushindi wa kwanza kwa upande wa wanawake umekwenda kwa Wizara Maji, nafasi ya pili Wizara ya Afya na nafasi ya tatu imekwenda kwa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi) wakati kwa upande wa wanaume nafasi ya kwanza imeenda kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nafasi ya pili Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Uchukuzi) na nafasi ya tatu imekwenda kwa Wizara ya Afya.

Nao mabingwa watetezi kwenye mchezo wa kuvuta kamba wanaume timu ya Idara ya Mahakama wamevuliwa ubingwa kwa kuvutwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi) kwa mivuto 2-1, katika mechi ya robo fainali iliyofanyika kwenye uwanja wa Shule ya Ufundi ya Tanga.

Mchezo huo ulikuwa mkali na wakuvutia ambapo katika mivuto miwili ya kwanza timu hizo zilitoka sare kwa kuvutana mvuto 1-1, na ndipo ukaongezwa mvuto wa tatu na ndipo Sekta ya Uchukuzi wanaibuka washindi na kutinga hatua ya nusu fainali.

Timu nyingine zilizoshinda kwa mivuto 2-0 kwa wanaume ni Wizara ya Mambo ya Ndani wamewavuta Wizara ya Maliasili na Utalii; huku Wizara ya Mifugo na Uvuvi waliwachapa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; na Ofisi ya Rais Ikulu waliwavuta Wizara ya Kilimo.

Kwa upande wa wanawake timu zilizoshinda kwa mivuto 2-0 na zote zimeingia hatua ya nusu fainali ni Idara ya Mahakama waliwavuta RAS Iringa; huku Ofisi ya Waziri Mkuu Sera wamewashinda Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI); nao Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi) waliwaliza Wizara ya Madini; wakati Wizara ya Maji waliwavuta Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa mvuto 1-0.

By Jamhuri