Bendi ya Muziki wa dansi ya Extra Bongo ya jijini Dar es Salaam inajipanga kuhakikisha inafanya maonesho ya kusisimua wakati wa kusherehekea Sikukuu ya Idd.

Kiongozi wa Bendi hiyo, Ali Choki amesema kuwa kwa sasa wanajifua ipasavyo waweze kuwapa raha wapezi wa bendi hiyo na kwamba watakuwa na staili mpya ya kushambulia jukwaa tofauti na mashabiki walivyozea kuwaona kila siku.

 

Bendi ya Extra Bongo chini ya Choki, ni mojawapo ya bendi za muziki wa dansi hapa nchini ambazo zimefanikiwa kuvuna idadi kubwa ya mashabiki kutokana na ubunifu wa aina mbalimbali katika kutoa burudani ya muziki huo.

 

“Muziki ni ushindani lakini pia ubunifu ni jambo la muhimu sana, kinachofanyika sasa hivi ni kuhakikisha kwamba mashabiki wetu wanatuona kivingine kabisa, hili linawezekana wala halina ubishi,” amesisitiza Choki.

 

Amesema ratiba ya maonesho ya bendi hiyo kwa ajili ya Sikukuu ya Idd itatolewa hivi karibuni baada ya kukamilisha maandalizi muhimu.

By Jamhuri